Gavana ahalalisha bangi bila ya kupiga kura

Muktasari:

Gavana huyo amesema mambo wanayofanya watu wazima vyumbani na majumbani mwao ni chaguo lao ili mradi hayaathiri watoto na afya ya wengine.

Kwa mara ya kwanza, jimbo la Marekani limehalalisha bangi kwa kuweka saini na si kwa kupiga kura.

Gavana wa jimbo la Vermont, Phil Scott amesaini muswada wa sheria namba 511 (House Bill 511) ambao unahalalisha kumiliki bangi za uzito usiopungua wakia moja na kuondoa adhabu za makosa ya kumiliki mimea iliyokomaa isiyozidi miwil au miine ambayo haijakomaa.

Hata hivyo, sheria hiyo haizungumzii lolote kuhusu kuanzishwa kwa soko kwa ajili ya mmea huo. Sheria hiyo itaanza kufanya kazi Julai, imeandika yahoo.com ikikariri tovuti ya HuffPost.

“Leo, kwa hisia tofauti, nimesaini H. 511,” alisema Scott katika taarifa aliyoituma kwa Bunge la jimbo hilo.

"Binafsi naamini kwamba ambayo ambayo watu wazima wanafanya ndani na kwenye nyumba zao ni chaguo lao, ili mradi tu hayana athari hasi kwa afya na usalama kwa wengine, hasa watoto.”

Kwa saini hiyo ya Scott, Vermont itaungana na majimbo mengine nane yaliyohalalisha bangi, ikiwa ni pamoja na Washington, D.C., katika wimbi linaloendelea kukua kufanya maamuzi yanayopingana na serikali ya shirikisho.

Serikali ya Marekani bado inaiweka bangi  katika jedwali la kwanza la madawa, ikiwa pamoja na dawa ya kulevya aina ya heroin na LSD.

Vermont ilihalalisha matumizi ya bangi kwa matibabu mwaka 2004, na sasa ni miongoni mwa majimbo 30, pamoja na nchi za Guam na Puerto Rico, na Wilaya ya Columbia, zilizohalalisha bangi kwa ajili ya matibabu.

Ingawa majimbo mengine yamehalalisha bangi kwa kutumia kura ili wananchi waamue, Vermont hairuhusu mchakato kama huo, badala yake wabunge wa jimbo hilo wamekuwa wakishughulikia suala hilo kwa kutaka mabadiliko ya sheria.

Muswada kama huo uliwasilishwa mezani kwa Scott mwaka jana, lakini alikataa kuupitisha, akisema kulikuwa na matatizo katika lugha iliyotumika katika adhabu kwa watakaobainika kuuza bangi kwa watoto na uanzishwa wa kamisheni kwa ajili ya kutafiti jinsi sheria sheria za kusimamia soko la bangi zitakavyofanya kazi katika jimbo hilo.