Mavunde aicharukia Halmashauri ya Sikonge

Muktasari:

Aitaka kukirejesha serikalini kituo cha vijana cha Tulu


Sikonge. Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana na Ajira), Anthony Mavunde ameiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge mkoani Tabora kuanza mchakato wa kukirudisha serikalini kituo cha vijana cha Tulu ambacho kinamilikiwa na asasi ya Pathfinder.

Amesema haiwezekani asasi isiyo ya kiserikali itumie fedha za Serikali, akitaka mchakato huo uanze mara moja ili kirudi Serikalini, lakini akataka vijana wapatao 36 waliopo kituoni hapo wawekwe kwenye mpango wa kunufaika na kituo hicho kitakaporudishwa serikalini badala ya kufukuzwa.

Akizungumza leo Julai 18, 2018 katika kituo hicho kilichopo Kata ya Igigwa, Mavunde alisema anashangazwa kuona kituo kinapewa na Serikali Sh1.8 bilioni halafu matumizi yake hayaeleweki.

Mavunde alisema kiasi kinachodaiwa kutumiwa ni kikubwa na kutaka uchunguzi wa kina ufanyike kujua matumizi ya fedha hizo.

"Jengo kama là ukumbi na ofisi kumi kugharimu Sh200 milioni si sahihi. Ingawa mimi si mhandisi, lakini kwa macho unaona," amesema.

Mavunde ameonyesha masikitiko yake kwa kituo hicho kutumika vibaya huku viongozi wakihusika kuvuruga malengo ya kituo hicho ya kuwapa vijana mafunzo ya ujuzi kama ushonaji, ufundi useremala na uashi.