Mboni Masimba aja na Sauti ya Mwanamke

Mtangazaji wa Kipindi cha "The Mboni Show" kinachoruka kupitia kituo cha televisheni TBC1, Mboni Masimba

Muktasari:

Katika  kongamano hilo litakalofanyika mkoani Mwanza Novemba 6, mwaka huu katika Hoteli ya Gold Crest,  wanawake mbalimbali waliofanikiwa kiujasiriamali, kibiashara na kielimu watakuwepo kuzungumza na wanawake  wa jiji hilo kwa kiingilio cha Sh40,000.

Mtangazaji wa Kipindi cha "The Mboni Show" kinachoruka kupitia kituo cha televisheni TBC1, Mboni Masimba ameandaa kongamano la kuwahamasisha wanawake aliloliita  Sauti ya Mwanamke lenye lengo la kuwapa uwezo wa kujikomboa kiuchumi.

Katika  kongamano hilo litakalofanyika mkoani Mwanza Novemba 6, mwaka huu katika Hoteli ya Gold Crest,  wanawake mbalimbali waliofanikiwa kiujasiriamali, kibiashara na kielimu watakuwepo kuzungumza na wanawake  wa jiji hilo kwa kiingilio cha Sh40,000.

Masimba anasema kwa kiingilio hicho wanawake wa Mwanza

 watapata elimu, burudani pamoja na chakula.

"Atakuwepo Shekha Nasser ambaye ni mmiliki wa Shear Illusion na Mwanzilishi wa Manjano Foundation huyu amefanikiwa sana kwenye biashara, atakuwepo Mkandarasi Maida Waziri pamoja na Biubwa Ibrahim ambaye ana Kampuni ya  Namaingo Agri_Busness Agency inayowawezesha watu mbalimbali katika masuala ya kilimo," amefafanua Masimba.

Anaongeza kuwa pamoja na kupata elimu ya biashara na ujasiriamali, maarifa kuhusu maisha na nyumba yatatolewa na wawezeshaji maarufu Bi Chau na Bi Fatma.

“Wanawake mnapokutana lazima mbadilishane ujuzi wa kila aina, hatutawaacha hivi hivi wanawake wa Mwanza, tumemuandaa Bi Chau na Bi Fatma kuwafunda yale mambo yetu,” anafafanua.

Shughuli yoyote ya wanawake bila burudani haiwezi kunoga ndiyo maana Masimba anawapeleka Mwanza, Isha Mashauzi na mchekeshaji Katarina Karatu kuifanya siku hiyo iwe nzuri.

Masimba anasema sherehe itaendeshwa na mshereheshaji maarufu nchini Mc Zipompapompa.

“Tunaanzia Mwanza, lakini kongamano letu litakwenda nchini kote, tunataka kuwakomboa kifikra wanawake wa Kitanzania, Sauti ya Mwanamke ni  sauti ya jamii, ipewe nafasi,” anasema Masimba.