Mbowe: Bajeti haitekelezeki, tutaipinga

Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe

Muktasari:

  • Amesema mapendekezo ya bajeti hiyo ya Sh31.6 trilioni yaliyowasilishwa juzi na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango hayawezi kutekelezeka kwa sababu hata ya mwaka huu wa fedha ni asilimia 34 ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo zimetolewa.
  • Akifungua mkutano wa Baraza la Uongozi la Chadema Kanda ya Kaskazini uliofanyika jijini hapa, Mbowe (pichani) alisema katika kikao cha kamati kuu ya chama hicho kilichofanyika jana wameweka msimamo kuwa bajeti hiyo haina msaada wowote kwa wananchi hasa wa hali ya chini.

Tanga. Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe amesema watakwenda bungeni kupinga bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha wa 2017/18 kwa kuwa haitekelezeki.

Amesema mapendekezo ya bajeti hiyo ya Sh31.6 trilioni yaliyowasilishwa juzi na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango hayawezi kutekelezeka kwa sababu hata ya mwaka huu wa fedha ni asilimia 34 ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo zimetolewa.

Akifungua mkutano wa Baraza la Uongozi la Chadema Kanda ya Kaskazini uliofanyika jijini hapa, Mbowe (pichani) alisema katika kikao cha kamati kuu ya chama hicho kilichofanyika jana wameweka msimamo kuwa bajeti hiyo haina msaada wowote kwa wananchi hasa wa hali ya chini.

“Kambi ya upinzani bungeni tunakwenda kupinga bajeti hiyo kwa sababu tunaamini fedha hizo hazitapatikana kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo,” alisema Mbowe.

Mwenyekiti huyo alisema mwaka jana wabunge wa kambi ya upinzani walieleza wazi kwamba bajeti ya mwaka huu isingetekelezeka na ndivyo ilivyotokea kwa sababu kati ya Sh11.8 trilioni zilizotengwa kwa shughuli za maendeleo ni Sh3.97 trilioni pekee zilizotolewa ikiwa ni asilimia 34 pekee.

“Angalau hata ingefikia asilimia 75 kungekuwa na matumaini, lakini hali halisi inaonyesha Serikali haina fedha na imeweka bajeti bila kuangalia uhalisia, matokeo yake hadi kipindi cha mwaka wa fedha kinamalizika halmashauri zinajikuta hazijafikishiwa fedha za kutekeleza shughuli za maendeleo,” alisema Mbowe.

Mbali ya bajeti, Mbowe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chadema, alitoa rai kwa Rais John Magufuli kuhusu hali ya kisiasa nchini akieleza kwamba baadhi ya matamko yanaweza kuwakimbiza wawekezaji, hivyo kusababisha kuporomoka kwa uchumi.

Pia alizungumzia suala la utoaji na upatikanaji wa taarifa akisema “Ushauri wa bure, Rais awaache wananchi wazungumze, anastahili kusikiliza vilio vya wananchi wake, awe mwepesi kusikiliza kuliko kujibu. Wananchi wasiposema mawe yatasema.”

Chadema ni Maalim Seif

Awali, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema (Bara), John Mnyika alieleza msimamo wa chama hicho uliowekwa katika kikao cha Kamati Kuu kuwa kinamtambua Maalim Seif Sharif Hamad kuwa ndiye katibu mkuu wa CUF na hakitashirikiana na Magdalena Sakaya.

“Tunatambua kuwa Profesa Ibrahim Lipumba amepewa jukumu la kuiua CUF, sisi Chadema hatuwezi kukubali kwa kuwa itaua Ukawa na baadaye Chadema,” alisema Mnyika.

Alisema chama hicho kitapambana kuhakikisha CUF haipasuki.