Mbowe: Tunajiandaa kukamata dola

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha Baraza Kuu la chama hicho kilichofanyika mjini Dodoma jana. Picha na Anthony Siame

Muktasari:

Kwa mujibu wa Mbowe, Chadema imefanya hivyo kutokana na maandalizi yao ya kushika dola mwaka 2020 na kuwa ndiyo maana wameanza kufanya hivyo mapema.

Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema wamebadili msingi wa uongozi wao ikiwamo kufanya mfumo unaoendana na mwaka wa Serikali ambao unaanzia Julai Mosi hadi Juni 30.

Kwa mujibu wa Mbowe, Chadema imefanya hivyo kutokana na maandalizi yao ya kushika dola mwaka 2020 na kuwa ndiyo maana wameanza kufanya hivyo mapema.

Akifungua mkutano wa Baraza Kuu mjini Dodoma jana, Mbowe aliwataka wajumbe na wanachama kukubaliana na mabadiliko hayo kutokana na hali ilivyo kwa sasa baada ya kuona chama kinakwenda vizuri na kinazidi kukua kila kukicha.

“Nasisitiza kuwa, lazima chama hiki tukilinde na kukijenga kwa gharama zote, tumepita milima na mabonde lakini ukweli hata ninyi mnajua kuwa tuko mahali salama sasa,” alisisitiza.

Awali, Katibu Mkuu wa Chadema Dk Vicent Mashinji alisema chama kinakua kwa kasi ya ajabu ambayo wengi wanashindwa kuijua.

Alisema kwamba mpango walionao ni kuhakikisha kuwa mwaka 2020 wanashika dola au kugawana wabunge nusu kwa nusu na chama tawala na akaomba Watanzania kutumia mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kuomba safari ya kushika dola iwe njema. Jumla ya wajumbe walioshiriki mkutano walikuwa 332 kati ya wajumbe halali 370.