Mbowe asema Chadema haitatetereka

Muktasari:

Amesema kuna mkakati mkubwa unaotumia fedha unaofanywa kuwalaghai viongozi na wanachama wake kukihama chama hicho.

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe amesema chama hicho hakiwezi kutetereka au kufa kwa kiongozi au mwanachama wake kuondoka.

Amesema kuna mkakati mkubwa unaotumia fedha unaofanywa kuwalaghai viongozi na wanachama wake kukihama chama hicho.

Kauli hiyo ameitoa leo Jumatano baada ya aliyekuwa mwenyekiti wa vijana wa chama hicho, Patrobas Katambi kutangaza kujiunga na CCM.

Akizungumza leo Jumatano na Mwananchi, Mbowe ambaye pia ni amesema, "Tuko ‘strong enough’ sio mara ya kwanza watu kuondoka hivyo wanachama wetu wasiogope waendelee kujenga chama na kuendelea na kampeni za udiwani,"

"Huiwezi kututeteresha, kuondoka kwa Katambi si hivi hivi, ushawishi wa fedha umetumika...ingawa ni haki yao ila hao hawaondoki kwa mapenzi yao na hilo halina ubishi,"

"Badala ya nguvu na fedha kuzielekeza kujenga viwanda wao nguvu wamezielekeza kushawishi viongozi wetu, wamewashawishi wengi na Katambi ni miongoni ingawa wengine wamekataa."

Mbowe amesema, "Katambi alikuwa katika majukumu ya chama na aliwaaga wenzake anakwenda kumuguza mama yake mgonjwa hivyo akakatiwa tiketi ya ndege, kumbe alikuwa anakwenda kukamilisha dili ambalo naambiwa limetumia saa 48 kukamilika."

Amesema Chadema ilipofika haiwezi kufa kwani imejijenga na hapo walioondoka lakini mpaka sasa kimeendelea kuwapo.

Mbowe amesema mwitikio wa wananchi katika kampeni za udiwani kwenye kata 43 umeishtua CCM ikiwamo kuhama kwa aliyekuwa mbunge wa Singida Kaskazini, Lazaro Nyalandu.