Mbunge Nachuma ataka uvumi juu yake upuuzwe

Muktasari:

  • Nachuma amesema wanaosambaza taarifa wana nia mbaya ya kumchafua kwa masilahi binafsi.

Mbunge wa Mtwara Mjini (CUF), Maftaha Nachuma amewataka wananchi wa jimbo hilo kupuuza taarifa zinazosambaa kwamba ana mpango wa kujiondoa katika chama hicho.

Amesema anaendelea kuwatetea wakazi hao ili wapate maendeleo.

“CUF hawana historia ya kuhamahama vyama, hata huyo aliyeondoka ameondoka kwa masilahi binafsi. Mimi Maftaha Nachuma nitakuwa wa mwisho kuondoka CUF,” amesema alipozungumza na MCL Digital leo Jumatano Desemba 6,2017.

Amesema suala la wabunge kujitoa katika nafasi zao linasababishwa na njaa kutokana na kuangalia masilahi binafsi bila kutetea wananchi.

Nachuma amesema wabunge wengi walidhani wakipata nyadhifa hizo watakuwa wananufaika kwa kupata fedha lakini sasa hilo halipo kwa kuwa ubunge siyo dili bali ni kwa ajili ya kuwatumia wananchi.

Kupitia mitandao ya kijamii imeelezwa kwamba mbunge huyo ana mpango wa kujiondoa CUF na kujiunga na CCM.

Nachuma amesema wanaosambaza taarifa hizo wana nia mbaya ya kumchafua kwa masilahi binafsi.