Mchakato vitambulisho vipya vya Taifa Oktoba 3

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Angella Kairuki akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari jana Dar es Salaam. Picha na Said Khamis

Muktasari:

  • Katika mchakato huo, wizara hiyo itashirikiana na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida), ambayo itaratibu mchakato wote wa utambuzi, kuhakiki taarifa za watumishi  na kuchukua alama za vidole.

Dar es Salaam. Wizara ya Utumishi na Utawala Bora iliyo chini ya Ofisi ya Rais, imesema kazi ya uhakiki wa watumishi hewa itakwenda sambamba na utoaji wa vitambulisho vipya vya Taifa kwa watumishi wa umma.

Katika mchakato huo, wizara hiyo itashirikiana na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (Nida), ambayo itaratibu mchakato wote wa utambuzi, kuhakiki taarifa za watumishi  na kuchukua alama za vidole.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Angella Kairuki amesema mchakato huo utafanyika kwa wiki mbili kuanzia Oktoba 3 na utawahusisha watumishi wa wizara, taasisi za Serikali zinazojitegemea, tawala za mikoa, mamlaka za Serikali za Mitaa na mashirika ya umma.