Mdahalo wa wagombea wenza kuonyeshwa leo moja kwa moja

dondoo

Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya mdahalo wa Urais  Wachira Waruru jana alisema  kwamba matayarisho ya mijadala hiyo imekamilika.

 

Muktasari:

Hata hivyo kumegibikwa na utata kwamba huenda wagombea hao wasijitokeze

Nairobi. Mdahalo  wa wagombeaji wenza wa urais nchini Kenya  unafanyika leo   katika ukumbi wa Chuo cha Catholic University of Eastern Africa (CUEA).

Hata hivyo, haijafahamika kwamba  Naibu Rais William Ruto atashiriki mdahalo huo kwani awali ripoti ambazo hazikuthibitishwa zilisema kuwa hatahudhuria.

Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya mdahalo wa Urais  Wachira Waruru jana alisema  kwamba matayarisho ya mdahalo huo yamekamilika.

“Tuliwaalika wagombeaji wote na tunataraji kuwa wote watafika kesho kushiriki mdahalo. Hii ni licha ya kwamba wote hawajatujibu kusema ikiwa watakuja au hawatakuja.” Alisema  Waruru

“Bado kuna muda kwa wao kuthibitisha lakini kama kamati tuko tayari kwa mdahalo huo,” alisema

Mbali na   Ruto  mgombea mwenza wa mgombea urais wa NASA, Raila Odinga, Kalonzo Musyoka, wengine wanaotarajiwa kushiriki ni Moses Marango (mgombea mwenza wa Joseph Nyaga) na Titus Ng’etuny (mgombea  mwenza wa Abduba Dida).

Wengine ni;  Emmanuel Nzai (mgombea mwenza wa Ekuru Aukot), Miriam Mutua (mgombea mwenza wa Michael Wainaina) na Eliud Kariara (mgombea mwenza wa Japheth Kavinga).

Wiki  iliyopita , kamati hiyo ililazimika kuahirisha mdahalo wa urais kutoka Julai 10 hadi Julai 24 baada ya Rais Uhuru Kenyatta na  Odinga kusema hawatashiriki kwa kutojulishwa mambo fulani kuhusu maandalizi.

Akithibitisha kuwa Rais hatashiriki, Katibu Mkuu wa chama cha Jubilee Raphael Tuju alisema uamuzi huo ulifikiwa kwa sababu shughuli hiyo “ilikuwa ikipangwa na watu wasiojulikana kupitia matangazo magazetini”.

Baada ya saa chache,  Odinga pia alitao taarifa akisema hatahudhuria shughuli hiyo. Lakini  alibadili msimamo na kusema yuko tayari kukabiliana na Rais Kenyatta kujadili  mambo muhimu  yenye umuhimu kwa taifa la Kenya.

“Tungependa kufafanua kwamba wanachama wa Kamati  ya maandalizi ya midahalo ya urais wamekuwa wakiwasiliana kila mara na timu zinazoshirikisha kampeni za wagombea hao hata kabla ya tarehe hiyo kutangazwa  Mei,” kamati hiyo ilisema kwenye taarifa iliyotiwa saini na  Waruru.

Juzi,  Waruru alishikilia  msimamo wake  kuwa mdahalo wa urais bado utafanyika kama ulivyoratibiwa upya  Julai 24.“Mdahalo wa Urais utaendelea ulivyoratibiwa, hamna mabadiliko yoyote,” akakariri.

Midahalo hiyo itarushwa  moja kwa moja katika vyombo vya habari vya nchini humo.