Mdahalo wa wagombea wenza kuonyeshwa leo moja kwa moja
Muktasari:
Hata hivyo kumegibikwa na utata kwamba huenda wagombea hao wasijitokeze
Nairobi. Mdahalo wa wagombeaji wenza wa urais nchini Kenya unafanyika leo katika ukumbi wa Chuo cha Catholic University of Eastern Africa (CUEA).
Hata hivyo, haijafahamika kwamba Naibu Rais William Ruto atashiriki mdahalo huo kwani awali ripoti ambazo hazikuthibitishwa zilisema kuwa hatahudhuria.
Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya mdahalo wa Urais Wachira Waruru jana alisema kwamba matayarisho ya mdahalo huo yamekamilika.
“Tuliwaalika wagombeaji wote na tunataraji kuwa wote watafika kesho kushiriki mdahalo. Hii ni licha ya kwamba wote hawajatujibu kusema ikiwa watakuja au hawatakuja.” Alisema Waruru
“Bado kuna muda kwa wao kuthibitisha lakini kama kamati tuko tayari kwa mdahalo huo,” alisema
Mbali na Ruto mgombea mwenza wa mgombea urais wa NASA, Raila Odinga, Kalonzo Musyoka, wengine wanaotarajiwa kushiriki ni Moses Marango (mgombea mwenza wa Joseph Nyaga) na Titus Ng’etuny (mgombea mwenza wa Abduba Dida).
Wengine ni; Emmanuel Nzai (mgombea mwenza wa Ekuru Aukot), Miriam Mutua (mgombea mwenza wa Michael Wainaina) na Eliud Kariara (mgombea mwenza wa Japheth Kavinga).
Wiki iliyopita , kamati hiyo ililazimika kuahirisha mdahalo wa urais kutoka Julai 10 hadi Julai 24 baada ya Rais Uhuru Kenyatta na Odinga kusema hawatashiriki kwa kutojulishwa mambo fulani kuhusu maandalizi.
Akithibitisha kuwa Rais hatashiriki, Katibu Mkuu wa chama cha Jubilee Raphael Tuju alisema uamuzi huo ulifikiwa kwa sababu shughuli hiyo “ilikuwa ikipangwa na watu wasiojulikana kupitia matangazo magazetini”.
Baada ya saa chache, Odinga pia alitao taarifa akisema hatahudhuria shughuli hiyo. Lakini alibadili msimamo na kusema yuko tayari kukabiliana na Rais Kenyatta kujadili mambo muhimu yenye umuhimu kwa taifa la Kenya.
“Tungependa kufafanua kwamba wanachama wa Kamati ya maandalizi ya midahalo ya urais wamekuwa wakiwasiliana kila mara na timu zinazoshirikisha kampeni za wagombea hao hata kabla ya tarehe hiyo kutangazwa Mei,” kamati hiyo ilisema kwenye taarifa iliyotiwa saini na Waruru.
Juzi, Waruru alishikilia msimamo wake kuwa mdahalo wa urais bado utafanyika kama ulivyoratibiwa upya Julai 24.“Mdahalo wa Urais utaendelea ulivyoratibiwa, hamna mabadiliko yoyote,” akakariri.
Midahalo hiyo itarushwa moja kwa moja katika vyombo vya habari vya nchini humo.