Meja Jenerali mstaafu ajeruhiwa kwa risasi

Muktasari:

  • Vijana waliokuwa kwenye bodaboda walimfuatilia na kumpiga risasi.

Dar es Salaam. Watu wanaosadikiwa kuwa majambazi wamemjeruhi kwa risasi Meja Jenerali mstaafu, Vincent Mritaba na kumpora Sh5 milioni.

Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema Meja Jenerali Mritaba alipigwa risasi jana Jumatatu jioni nje ya nyumba yake Mbezi Beach jijini Dar es Salaam.

Amesema Meja Jenerali Mritaba alifikwa na mkasa huo akitoka kuchukua fedha katika Benki ya NMB tawi la Tangi Bovu.

“Vijana waliokuwa na bodaboda walikuwa wakimfuatilia muda mrefu na alipofika getini walimfyatulia risasi na kumjeruhi tumboni na bega la kulia,” amesema.

Kamanda Mambosasa amesema Meja Jenerali Mritaba amelazwa katika Hospitali ya Jeshi Lugalo anakoendelea na matibabu.