Muktasari:

Ripoti kutoka huko Bernabeu zinafichua kwamba wamepanga kupeleka ofa ya maana mwishoni mwa msimu huu ili kumng'oa Coutinho Anfield huku wakitambua wazi kwamba watakuwa kwenye vita kubwa na mahasimu wao, Barcelona ambao wanapiga hesabu pia za kumsajili syaa huyo wa zamani wa Inter Milan.

Madrid, Hispania. REAL Madrid imetangaza vita rasmi kwamba itapigana kwa nguvu zote katika kuiwania saini ya kiungo wa Liverpool, Mbrazili Philippe Coutinho.

Ripoti kutoka huko Bernabeu zinafichua kwamba wamepanga kupeleka ofa ya maana mwishoni mwa msimu huu ili kumng'oa Coutinho Anfield huku wakitambua wazi kwamba watakuwa kwenye vita kubwa na mahasimu wao, Barcelona ambao wanapiga hesabu pia za kumsajili syaa huyo wa zamani wa Inter Milan.

Real Madrid wanaonolewa na Mfaransa Zinedine Zidane wanaonekana kupania kwenye mchakato huo wa kuipata saini ya Coutinho baada ya kufikiria hata kuwapiga bei viungo James Rodriguez na Isco ili kupata Pauni 70 milioni ambazo zitatosha kupeleka ofa yao Anfield.

Staa wa Chelsea, Eden Hazard ni mchezaji mwingine aliyekuwa kwenye rada za Real Madrid ambao wamepanga kukifanyia marekebisho makubwa kikosi chao mwisho wa msimu huu ili kurejea kwa kasi kubwa msimu ujao. Chelsea hawana mpango wa kumuuza nyota wao huyo, lakini Madrid wanaamini hakuna kinachoshindikana kwenye pesa.

Barca wanamtaka Coutinho hasa baada ya Mbrazili wao Neymar kudai kwamba anapenda apate nafasi ya kucheza pamoja na Coutinho huko Nou Camp.