Kichuya na wenzake kuifuata Kagera baada ya mechi

Shiza Kichuya

Muktasari:

  • Wachezaji hao ni Said Ndemla, Muzamiru Yassin, Jonas Mkude, Abdi Banda, Ibrahim Ajib, Mohammed Hussein ‘Shabalala’ na Shiza Kichuya ambao walikuwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichocheza mechi za kimataifa za kirafiki dhidi ya Botswana na Burundi.
  • Akizungumza na gazeti hili, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara alisema uongozi umejipanga kuhakikisha timu hiyo inavuna pointi zote tisa kanda ya ziwa.

Dar es Salaam.Nyota saba wa Simba waliokoa kwenye kikosi cha Timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ wanaondoka Jumatano Machi 29 kwenda Kagera kujiunga na wenzao waliopo mkoani humo kujiandaa na mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Kagera Sugar utakaochezwa Jumapili Aprili 2 kwenye Uwanja wa Kaitaba.

Wachezaji hao ni Said Ndemla, Muzamiru Yassin, Jonas Mkude, Abdi Banda, Ibrahim Ajib, Mohammed Hussein ‘Shabalala’ na Shiza Kichuya ambao walikuwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichocheza mechi za kimataifa za kirafiki dhidi ya Botswana na Burundi.

Akizungumza na gazeti hili, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara alisema uongozi umejipanga kuhakikisha timu hiyo inavuna pointi zote tisa kanda ya ziwa.

“Tuna mechi tatu ngumu kwa kuanza na mchezo dhidi ya Kagera Sugar, dhamira yetu ni kutopoteza mchezo wowote,”alisema Manara

Simba inayoongoza Ligi Kuu kwa kuwa na pointi 55 na ikiwa imedhamiria kutwaa ubingwa msimu huu haina budi kushinda michezo hiyo na inapaswa kuiombea mabaya Yanga yenye pointi 53 ili iteleze kwenye michezo yake ijayo vibaya.

Kocha Msaidizi wa Simba,Jackson Mayanja alisema mchezo dhidi ya Kagera ni mkubwa lakini hawana presha kwa kuwa kikosi chake kimekamilika kila idara.

“Tuliteleza kwenye mechi na Mbeya City lakini Yanga walishindwa kuitumia, kama wangeshinda dhidi ya Mtibwa ingekuwa presha kwetu lakini huu ni mpira na tunafikiria zaidi kuhusu mechi za kanda ya ziwa.

“Yanga pia wana mchezo wa Azam na ambao ni mgumu kwao. Kilicho muhimu kwetu ni kupata ushindi mkubwa kwenye mechi zote tutakazocheza huku (Kanda ya Ziwa),”alisema Mayanja, aliyewahi kuwa mchezaji wa zamani wa timu ya Taifa ya Uganda ‘Uganda Cranes’.

Hata hivyo, Simba itaendelea kumkosa beki wake Method Mwanjale ambaye bado hajapona tangu alipoumia kwenye mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Prisons.