Mapato Yanga, AFC yameibwa, ngumi zatembea

Muktasari:

Katika mchezo huo ambao Yanga ilibuka na ushindi wa mabao 3-0, uliandaliwa kwa zaidi ya Sh 20 milioni, lakini waandaji hao waliambulia Sh 6.2 milioni kinyume na matarajio yao.

Arusha: Mchezo wa kirafiki kati ya Mabingwa wa Ligi Kuu Bara Yanga dhidi ya AFC Arusha umezaa balaa baada ya kutokea mzozo katika chumba cha kuhesabia fedha.

Katika mchezo huo ambao Yanga ilibuka na ushindi wa mabao 3-0, uliandaliwa kwa zaidi ya Sh 20 milioni, lakini waandaji hao waliambulia Sh 6.2 milioni kinyume na matarajio yao.

Kutokana na hali baadhi ya wajumbe walipiga hesabu hiyo wakiwashutumu wenzao wakuwaiba jambo lililozua mzozo na kutaka kupigana.

Mmoja wa wanakamati waandaji wa mchezo hakutaka kutajwa jina lake alisema baada ya kuona mapato madogo ndipo mzozo mkubwa ulitokea chumbani na watu kushikana mashati kwa madai wenzao wameiba fedha hizo.

 

“Inavyoonekana kulikuwa na tiketi feki ambazo zilitengenezwa na wachache wetu kwaajili ya kujipatia fedha kwa maana haiwezekani umati wote ule ipatikane milioni sita tu”

Awali waandaji walitangaza kiingilio cha jukwaa kuu  ni Sh20,000, eneo la mzunguko Sh 10,000, lakini kutokana na mashabiki wengi kushindwa kumudu kiwango hicho ndipo tiketi hizo zikaanza  Sh10,000 hadi 5,000, pamoja na kushuka wa bei hiyo ya tiketi bado hali haikuwa nzuri na kufanya tiketi kushushwe tena kutoka 5,000 kwa mtu mmoja na kufanya watu wawili kujichanga Sh 2,500 kila mmoja ili kununua tiketi moja.

Hali hiyo kukasababisha mapato kupatikana chini ya matarajio ya waandaji ambao waliambualia Sh 6.2 milioni.

Mwenyekiti wa AFC, Charles Mnyalu alisema wamepata kiasi kidogo cha fedha kutokana na kuuza tiketi  za Sh 20000, ambazo hazikufika hata 5,000.

“Ukweli uliopo ni hasara tumeambulia maana mchezo ule uliandaliwa kwa zaidi ya Sh 20 milioni, tunaambulia fedha isiyofika Sh 10Mil, tutakapofanya mahesabu kamili pamoja na mgao kwa timu taarifa itakuwa wazi,” alisema Mnyalu.

xxxxxxxxxxx