Mechi ya Yanga na Ruvu Shooting yahamishiwa Chamazi

Muktasari:

  • Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa alisema mechi hiyo imehamishiwa Chamazi kutokana na Uwanja wa Taifa  kesho kutumika kwa shughuli za kiserikali.

 Mechi ya kirafiki ya Yanga na Ruvu Shooting iliyokuwa ichezwe kesho kwenye Uwanja wa Taifa sasa itachezwa kwenye Uwanja wa Chamazi.

Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa alisema mechi hiyo imehamishiwa Chamazi kutokana na Uwanja wa Taifa  kesho kutumika kwa shughuli za kiserikali.

"Tumepata taarifa  kutoka serikalini asubuhi kuwa Uwanja wa Taifa  kesho unatumika kwa shughuli za kitaifa hivyo hatutaweza kucheza mechi yetu hapo na kama unavyojua hatuwezi kubishana na Serikali.

"Tunaishukuru Azam kwa kutukubalia mechi yetu tuihamishie kwenye uwanja wao, hivyo tunawaomba mashabiki waje kwa wingi Chamazi kushuhudia mchezo huo kama walivyofanya katika mchezo uliopita," alisema Mkwasa.

Alisema katika mchezo huo viingilio vitakuwa Sh7,000 kwa VIP na Sh5,000 mzunguko.

Mkwasa alisema baada ya mchezo huo wa kesho, Yanga itaondoka Jumapili asubuhi kwenda Zanzibar na usiku itacheza mechi nyingine ya kirafiki  na Mlandege  itakayofanyika kwenye Uwanja wa Aman .

Alisema Jumatatu timu hiyo itaelekea Pemba kuweka kambi ya wiki moja kujiandaa na mechi ya Ngao ya Jamii dhidi ya Simba itakayofanyika Agosti 23.