Mhispania amkumbatia Bocco kuichezea Azam

Mshambuliaji wa Azam, John Bocco

Muktasari:

  • Wiki hii vyombo vya habari vilitawaliwa na taarifa kuwa Bocco hayupo katika mipango ya kocha Mhispania huyo na sasa anamtafutia kazi nyingine.
  • Hernandez alisema taarifa hizo ni uzushi na kwamba Bocco ni miongoni mwa wachezaji watakaosalia ndani ya timu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu.

Dar es Salaam. Kocha wa Azam,  Zebenzui Hernandez amezima kelele zilizozagaa kuwa John Bocco hana nafasi katika kikosi chake na kusema mshambuliaji huyo ataitumikia Azam msimu ujao.
Wiki hii vyombo vya habari vilitawaliwa na taarifa kuwa Bocco hayupo katika mipango ya kocha Mhispania huyo na sasa anamtafutia kazi nyingine.
Hernandez alisema taarifa hizo ni uzushi na kwamba Bocco ni miongoni mwa wachezaji watakaosalia ndani ya timu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu.
“Hizo ni taarifa potofu, mimi sijazungumza kuhusu kuachwa kwa Bocco na labda nikwambie yeye (Bocco) ni miongoni mwa wachezaji tegemeo wa kikosi hicho,” alisema.
Kuhusu mwenendo wa kikosi chake, Hernandez alisema anatarajia kuwasilisha ripoti yake kwa uongozi baada ya wiki moja na kusisitiza kikosi chake hakitazidi wachezaji 22.
“Nina wachezaji wazuri ingawa kwa kipindi kilichobaki najaribu kufanyia kazi baadhi ya mambo ili kuhakikisha timu yangu inakuwa fiti. Natetegemea kutokuwa na wachezaji wengi, nitakuwa na wachezaji wasiozidi 22. Sitaki kuwa na kundi kubwa la wachezaji,” alisema.
Azam iliyomaliza nafasi ya pili msimu uliopita itaelekea kisiwani Zanzibar kesho kuweka kambi ya wiki moja kujiandaa na Ligi Kuu.