RT yakiri kupeleka watalii Kenya

Dar es Salaam. Uongozi wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT) umekiri kushindwa kuiandaa timu ya riadha ya vijana kwa ajili ya mashindano ya dunia yaliyomalizika jana, Kenya na Tanzania kutoka kapa.

Mwanariadha, Shomari Mtalimu aliondoshwa siku ya kwanza ya mashindano hayo katika mchujo wa mbio za mita 1500 wakati Winfrida Makenji akiondoshwa siku mbili katika mchujo wa mbio za mita 200.

Katibu Mkuu wa RT, Wilhelim Gidabuday amesema RT haikuiandaa ipasavyo timu hiyo, lakini akataka shirikisho hilo lisilaumiwe kwa matokeo hayo kwa kile ambacho alieleza yote hayo yamechangiwa na ukata.

"Tulijaribu kuhangaika ili kupata ufadhili, tulikwenda kuomba Serikalini lakini kote tulikwama, tukalazimika kupeleka wanariadha wawili kati 12 waliokuwa wamefuzu, pia hawakufanya vizuri hiyo imechangiwa na maandalizi, lakini tumejifunza," alisema Gidabuday.

Timu hiyo imerejea leo baada ya kufungwa kwa mashindano hayo jana Jumapili jijini Nairobi Kenya.

Katika hatua nyingine, RT imetangaza kuhairishwa kwa mashindano ya taifa yaliyokuwa yafanyike Julai 22 na 23, Kibaha mkoani Pwani.

"Sababu kubwa iliyochangia kuahirishwa kwa mashindano hayo ni ukata, tumekuwa na mashindano mbalimbali mwaka huu ambayo yametumia fedha ikiwamo kuiweka kambini timu yetu itakayokwenda kwenye mashindano ya dunia Agosti kule Uingereza.

"Hivyo hatuna budi kuhairisha mashindano ya taifa hadi pale yatakapotangazwa tena," alisema Gidabuday.