Simba yatwaa ubingwa wa Ngao ya Jamii

PENALTI YA USHINDI YA SIMBA DHIDI YA YANGA KWENYE MECHI YA NGAO YA JAMII

Muktasari:

Kipa Manura aliyesajili na Simba akitokea Azam alithibisha ubora kwa kudaka penalti ya kwanza ya Yanga iliyopigwa na Kelvin Yondani.

Dar es Salaam. Kipa Aishi Manura na kiungo Mohamed Ibrahimu wameiongoza Simba kutwaa ubingwa wa Ngao ya Jamii kwa kuifunga Yanga kwa penalti 5-4.

Katika mchezo huo uliomalizika dakika 90 kwa timu hizo kutoka suluhu ndipo penalti zilipotumika kuamua bingwa wa mechi hiyo ya ufunguzi wa msimu mpya wa 2017-18.

Kipa Manura aliyesajili na Simba akitokea Azam alithibisha ubora kwa kudaka penalti ya kwanza ya Yanga iliyopigwa na Kelvin Yondani.

Wakati Mo Ibrahimu alifungia Simba penalti ya sita baada ya kiungo wa Yanga, Juma Mahadhi kuikosa penalti yake ya sita kwa kupaisha.

Wafungaji wa Simba katika penalti hizo ni nahodha Method Mwanjali, Emmanuel Okwi, Haruna Niyonzima, Shiza Kichuya wakati Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ akikosa kabla ya Mo Ibrahimu kufunga penalti ya sita.

Yanga ilianza penalti hizo vibaya kwa Kelvin Yondani na baadaye Juma Mahadhi kukosa huku walipopata ni nahodha Thaban Kamusoko, Pappy Tshishimbi, Ibrahimu Ajib, Donald Ngoma.

Simba ilianza mechi hiyo kwa kasi na kulishambulia lango la Yanga, lakini ngome ya mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara walikuwa imara tuliza presha hiyo.

Kiungo wa Yanga, Tshishimbi na beki Gabriel Michael walifanya kazi kubwa kutibua mipango ya Simba walionekana kuwa ni wazuri kwa pasi za chini hasa napokaribia langoni kwa wapinzani wao.

Ajib alifanya kile kilichosubiliwa na mashabiki wake kwa kuchezea mpira, lakini pasi zake za mwisho hazikuweza kumfikia Ngoma.

Wakati Simba, Niyonzima na  Kichuya walishindwa kabisa kumchezesha Laudit Mavugo jambo lililomfanya muda mwingi kukosa pasi nzuri za kulifikia lango la Yanga.