Simbu atua London na matumaini kibao

Arusha. Mwanariadha Alphonce Felix Simbu (24) amefika salama London tayari kwa kuiwakilisha Tanzania katika mashindano ya London marathoni yatakayofanyika Jumapili

Simbu amesema amefanikiwa salama na anatarajia kufanya makubwa kwa ajili ya heshima ya nchi yake sambamba na kufuta ukame wa medali katika mashindano makubwa duniani.

“Huu mwaka ni mwaka wa medali tu, Watanzania wafahamu sikuja London kushiriki wala kushangaa bali kushinda hivyo wajiandae na kupokea medali,”

Alisema Simbu na kuongeza kuwa anataka kutumia mashindano hayo katika maandalizi yake ya kuelekea katika mbio za duniani zitakazofanyika London, Agosti.

Katibu mkuu wa shirikisho la riadha nchini Wilhelm Gidabuday alisema Simbu ameondoka akiwa na matumaini makubwa ya kurejea na ubingwa hivyo ni faraja kwao pia.

“Simbu tayari amefikia viwango vya kushiriki mashindano ya kimataifa ataungana na Ezekiel Japhary aliyefikia viwango hivyo katika mbio za Hanover Marathon alipomaliza katika nafasi ya sita.”