Wachezaji wa timu za taifa za wanawake kutoka mataifa 20, wanapanda kileleni Mlima Kilimanjaro

Muktasari:

  • Wachezaji hao kutoka katika mataifa ya  Uingereza, Canada, Japan, Joldan, Nepal, Ujerumani, Marekani, Ufaransa, Afrika Kusini, Rwanda, Falme za Kiarabu na nchi nyingine wanatarajia kushuka mlima huo Juni 26, mwaka huu, kupitia lango la Marangu.

Wachezaji wa timu za Taifa za wanawake kutoka katika mataifa 20 duniani, wamepanda Mlima Kilimanjaro.

Wachezaji hao kutoka katika mataifa ya  Uingereza, Canada, Japan, Joldan, Nepal, Ujerumani, Marekani, Ufaransa, Afrika Kusini, Rwanda, Falme za Kiarabu na nchi nyingine wanatarajia kushuka mlima huo Juni 26, mwaka huu, kupitia lango la Marangu.

Wachezaji hao wameandamana na ujumbe wa watu zaidi ya watu 450, wakiwepo waongoza watalii 30, wapagazi 360 na wachezaji, makocha na wanahabari wa kimataifa 60.

Safari ya kupanda mlima huo ya wachezaji hao imeratibiwa na taasisi yao, Equal Playing Fied ilianza kupanda mlima huo, kupitia lango la Londorosi kwa kuongozwa na maafisa wa bodi ya Utalii nchini (TTB).

Afisa habari Mkuu wa bodi ya Utalii nchini, Geofrey Tengeneza, alisema safari ya wachezaji hao inatarajiwa kutangaza mlima Kilimanjaro kimataifa na kuvutia watalii.

"Ujumbe wa wachezaji hawa, umeambatana na vyombo vya habari vya kimataifa, una manufaa makubwa katika kukuza utalii na michezo hapa nchini."

Mratibu wa safari hiyo, Rajvi Ladha mchezaji wa zamani wa timu ya taifa ya wanawake Twiga Star, ambaye anayeishi nchini Dubai, alisema lengo la safari hiyo ni kutangaza mlima Kilimanjaro kupitia soka la wanawake duniani na pia kuinua soka la wanawake.

Ladha alisema, wanatarajia kucheza soka june 24 katika eneo la creta na tayari wameandaa timu mbili, Volcan FC na Clacier Fc hatua ambayo itaweza rekodi duniani.

Mchezaji wa timu ya taifa ya Canada, Sasha Andrews alisema katika ziara yao hapa nchini, pia wanakusudia kufanya cliniki ya mchezo wa soka la wanawake katika jiji la Arusha na Jiji la Dar es Salaam.