Wenger nitaondoka Arsenal

Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger

Muktasari:

Bosi huyo wa Gunners alipoulizwa kama anastahili kuendelea na kazi yake amesema suala la kustaafu ukocha mwaka huu hilo halipo na kwamba msimu ujao ataendelea na kazi yake hiyo iwe klabuni Arsenal au kwenye timu nyingine yoyote.

Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger amekiri kuwa anaweza kuachana na klabu hiyo mwisho wa msimu.
Bosi huyo wa Gunners alipoulizwa kama anastahili kuendelea na kazi yake amesema suala la kustaafu ukocha mwaka huu hilo halipo na kwamba msimu ujao ataendelea na kazi yake hiyo iwe klabuni Arsenal au kwenye timu nyingine yoyote.
Aliongeza: “Jambo muhimu ni klabu hiyo kuwa katika mikono salama, iwe ni mimi au mtu mwingine.”
Wenger alisema kama Arsenal wataamua kuachana naye mwishoni mwa msimu huu basi ataendelea kuwa kocha na atahamia kwenye timu nyingine hivyo ni suala la wakati tu inaweza kutokea akacheza dhidi   ya timu hiyo aliyoinoa kwa miaka 21 sasa.
Wenger ameingia katika wakati mgumu mbele ya mashabiki wa Arsenal baada ya timu hiyo kunyukwa mabao 5-1 katika Ligi ya Mabingwa na Bayern Munich juzi Jumatano.