Miili ya askari JWTZ kurejeshwa nchini leo

Muktasari:

Uvamizi huo ulifanyika katika kambi ndogo iliyopo katika daraja la Mto Simulike, kaskazini mashariki mwa Wilaya ya Beni.

Dar es Salaam. Miili ya askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) waliouawa na waasi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) inarejeshwa nchini leo.

Taarifa ya ofisi ya habari ya JWTZ imesema miili ya askari hao itawasili nchini leo Jumatatu Desemba 11,2017 saa kumi na mbili jioni katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA).

Awali, akizungumzia na waandishi wa habari jana Jumapili Desemba 10, 2017 Mnadhimu Mkuu wa JWTZ, Luteni Jenerali James Mwakibolwa alisema miili ya askari hao ingerejeshwa nchini kati ya Jumanne Desemba 12, au Jumatano Desemba 13,2017 kwa ushirikiano kati ya Serikali na Umoja wa Mataifa (UN).

Mwakibolwa alisema askari hao walivamiwa kambini na waasi wa ADF na mapigano yalidumu kwa takriban saa 13. Alisema askari 14 wa JWTZ waliuawa, 44 wamejeruhiwa na wengine wawili  hawajulikani walipo.

Alisema tukio hilo lililotokea Desemba 7,2017 katika kambi ndogo iliyopo katika daraja la Mto Simulike, kaskazini mashariki mwa Wilaya ya Beni, Jimbo la Kivu nchini DRC.