Mkurugenzi awafungia geti wachelewaji kazini

Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Kiomoni Kibamba.

Muktasari:

  • Tukio hilo lililodumu kwa nusu saa, limetokea saa 1.30 baada ya kufika ofisini hapo na kufunga geti ili kuwabaini wanaochelewa kazini.
  • Akizungumza ofisini kwake baada ya tukio hilo, Kibamba alisema lengo ni kujenga nidhamu ya kazi.

Mwanza. Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Kiomoni Kibamba amewafungia geti wafanyakazi wa ofisi hiyo kwa madai ya kuchelewa kufika kazini.

Tukio hilo lililodumu kwa nusu saa, limetokea saa 1.30 baada ya kufika ofisini hapo na kufunga geti ili kuwabaini wanaochelewa kazini.

Akizungumza ofisini kwake baada ya tukio hilo, Kibamba alisema lengo ni kujenga nidhamu ya kazi.

“Nimefika hapa 12.45 asubuhi, lakini sikuingia ofisini nilikaa nje, ilipofika saa 1.30 asubuhi nikafunga geti ili niwaone wote waliofika baada ya muda huo, ilipofika saa mbili nimewafungulia, nilikuwa nawashtua ili wafuate utaratibu wa kazi,” alisema.

Alisema kwa mujibu wa kanuni za kudumu za utumishi wa umma za mwaka 2009, muda wa kufanya kazi ni saa nane kwa siku na mtumishi anatakiwa kufika kazini saa 1.30 asubuhi na kuondoka saa 9.30 alasiri.