Moto waendelea kuwaka CCM

Muktasari:

  • Wiki iliyopita, Polepole alisema katika kipindi cha redio Times kuwa wanachama wanaotaka kugombea ubunge kwa tiketi ya CCM 2020, sasa watalazimika kuwa wakazi wa eneo wanalotaka kuliwakilisha, sharti ambalo linaweza kuwaondoa takriban nusu ya wabunge wa sasa.

Wakati Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole akiwataka wakuu wa wilaya nchini kuwa na hekima ya kuridhika na vyeo walivyonavyo moto umeendelea kuwaka ndani ya chama hicho, baadhi ya makada na wachambuzi wa siasa kukosoa pendekezo lake la wagombea kuwa wakazi wa majimbo husika.

Wiki iliyopita, Polepole alisema katika kipindi cha redio Times kuwa wanachama wanaotaka kugombea ubunge kwa tiketi ya CCM 2020, sasa watalazimika kuwa wakazi wa eneo wanalotaka kuliwakilisha, sharti ambalo linaweza kuwaondoa takriban nusu ya wabunge wa sasa.

Tamko hilo la Polepole lilizua mjadala mzito jambo lililosababisha Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM Organaizesheni, Pereira Silima alitoa taarifa kueleza kuwa hakuna mahali popote katika mabadiliko ya katiba yao palipoandikwa kuwa wagombea wa udiwani na ubunge watajadiliwa kwa sifa ya kuishi jimboni.

Ukiacha hilo juzi usiku katika kipindi cha ‘Tuambie’ kinachorushwa na televisheni ya TBC, Polepole alizungumzia suala jingine la kuwa kanuni za uchaguzi haziwakatazi wakuu wa wilaya kuwa wajumbe wa mkutano mkuu wa Taifa wa CCM, wanapaswa kuwa na hekima.

Kauli ya Polepole imekuja wakati tayari kukiwa na wakuu wa wilaya wanne, mkuu wa mkoa na makatibu tawala walioshinda katika chaguzi za chama hicho zilizofanyika hivi karibuni.

Walioshinda ni pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Halima Dendego ambaye aligombea ujumbe wa mkutano mkuu wa CCM baada ya kupata kura 311.

Mwingine ni Katibu Tawala wa Wilaya ya Nanyumbu, Salum Palango aliyepata kura 295.

Wakuu wa wilaya walioshinda ni Simon Odunga (Chemba) aliyeshinda kwa kura 432, Christina Mndeme (Dodoma) na Elizabeth Kitundu (Bahi) wote kutoka mkoani Dodoma.

Mkoani Morogoro, walioshinda ni Alhaji Mohamed Utaly (Mvomero) na Seriel Nchembe (Gairo).

Wakuu wengine wa wilaya walioshinda ni Raymond Mushi (Babati) mkoani Manyara, Herman Kapufi (Geita), katibu tarafa wa Makuyuni (Arusha), Paul Kiteleki na mkuu wa Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha, Alexander Mnyeti.

“Ukienda kwenye kanuni za uchaguzi za 2017 fungu la 25: Nafasi ya uongozi ni kazi ya muda wote (inazitaja hapo), Mkutano Mkuu wa Taifa haujatajwa, lakini mkuu wa wilaya ni kiongozi wetu wa Serikali pia ni kiongozi wetu wa chama,” alisema Polepole na kuongeza:

Mkuu wa wilaya ni mjumbe wa kamati ya siasa ya wilaya ni mjumbe wa halmashauri kuu ya wilaya na ni mjumbe wa mkutano mkuu wa wilaya. Huyu pia ni kamisaa wa Serikali, ‘public officer’ anayefanya kazi zote za chama. Sasa nikasema hekima pale ituongoze, yaani mtu ujiongeze mwenyewe.”

Aliendelea kusema: “Kama wewe una dhamana zote hizi, kwa nini mkutano mkuu tusimwachie mwanachama mwingine asiye na dhama nyingine yeye ashiriki kwenye mkutano wa chama?”

Polepole aliyewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Musoma mkoani Mara na baadaye Ubungo jijini Dar es Salaam alisema kwa sasa kuna wakuu wa wilaya wapatao 166 na kama wote wataomba nafasi hizo, watafurika kwenye nafasi za chama hicho.

“Kama wakuu wa wilaya wote watachukua kwa pamoja wako 166, zamani mkutano mkuu tulikuwa 2400 sasa hivi tumepunguza idadi tumekuwa 1,700, hao ni wanachama walioomba dhamana halafu kati ya hao 166 ni wakuu wa wilaya,” alisema Polepole na kuongeza:

“Upande wa pili ni hekima ya kuwa na kiasi. Wewe una nafasi kadhaa, hizi nafasi nyingine tumwachie mtu mwingine. Hiyo inakuja kutokana na maelekezo yetu kwenye fungu la 22 kwamba; mtu mmoja kofia moja. Ukiwa kiongozi una dhamana tayari basi hii nyingine waachie wengine nao waweke mawazo yao katika kupeleka mbele chama chetu.”

Mbunge wa Nzega Mjini(CCM), Hussein Bashe katika maoni yake alisema dhana ya ukazi imepitwa na wakati pamoja na kuwa inaenda kinyume na Katiba, kanuni na tamaduni za chama hicho.

“Nimeisikia kauli ya katibu wangu nadhani ni kauli ambayo inahitaji mjadala mpana, binafsi naamini chama chetu kina katiba, Kanuni na maadili. Utamaduni huu ndo msingi a chama chetu ambao unatuongoza,” alisema.

Bashe alisema dhana ya aina hiyo ikipewa fursa siku moja itakuja hoja ya kwamba anayetakiwa kugombea uchaguzi ni lazima awe mchaga, ikiwa hoja ya mkazi itakosa uhalali na nguvu kisiasa.

“Fursa aina hii ya mawazo ikipewa uhalali, siku moja hoja ya mkazi ikikosa uhalali na nguvu ipo siku tutatumia ukabila, ikiisha tutasema udini kwa kuwa ukiwa muislamu utayajua sana matatizo ya waislamu,” alisema.

Bashe alisema mbunge anayo majukumu yake nayo ni uwakilishi na kwamba, mbunge kuwa mkazi haiwezi kumfanya azifahamu shida za watu yapo mambo ya msingi ambayo yanatakiwa kutazwa.

“Je Mbunge ametimiza majukumu yake? Ametimiza ahadi zake? Amekuwa muwakilishi mzuri wa wananchi wake? Dhana hii binafsi naiona kama ni dhana ‘aoutdated’ (imepitwa na wakati),” alisema.

Alisema kuwa hoja ya mkazi haimfanyi mtu kuwa mwakilishi mzuri na ifahamike kwamba wabunge wengi wanafanya shughuli mbalimbali ikiwazo zao binafsi zinazosaidia maendeleo ya wananchi wake.

“Mwalimu Nyerere alitengeneza mifumo toka Tanu mpaka CCM ya kumuandaa kiongozi kuanzia Chipukizi, Yuth Legue.Haya ni maeneo ya majaribo na makosa

Alisisitiza kuwa zipo nafasi ambazo kiongozi hatakiwi kutoa kuli yenye Taswira ya kuwagawa watanzania kwa msingi wowote ule hata kama utakuwa na nia njema.

“Tumeona kauli ya Silima, ni kauli sahihi kabisa. Hivi karibuni kumekuwa na matamko controversial ambayo unajiuliza duh hivi Katibu Mkuu yupo wapi? Hata kama tunafanya reform, hii ni njia sahihi? Vitisho vimekuwa vingi sana,”alisema Bashe.

Alieleza kuwa CCM ni wanachama na wanachama

“Leo wana CCM wameanza kuwa wanyonge na hofu ya kukosa ari. Tumeanza kujenga tabaka la watawala na watawaliwa ndani ya chama, ni muhimu sana kila kiongozi aheshimu katiba na kupima kauli zetu,”.