Mshikemshike uchaguzi CCM wakolea mtandaoni

Muktasari:

Tangu mchakato wa uchaguzi huo uanze ngazi ya mashina, kata na mikoa wagombea waliokuwa wanateuliwa hawakuruhusiwa kufanya kampeni wala kusambaza vipeperushi na majina yao yalijulikana mbele ya mkutano wa uchaguzi.

       Dar es Salaam. Mshikemshike wa kampeni za uchaguzi ndani ya CCM ngazi ya taifa umeanza kushika kasi kwa wagombea kujinadi kupitia mitandao ya kijamii kabla ya Mkutano Mkuu wa Taifa utakaofanyika Desemba 18 na 19, mwaka huu.

Tangu mchakato wa uchaguzi huo uanze ngazi ya mashina, kata na mikoa wagombea waliokuwa wanateuliwa hawakuruhusiwa kufanya kampeni wala kusambaza vipeperushi na majina yao yalijulikana mbele ya mkutano wa uchaguzi.

Tofauti na ilivyokuwa kwa chaguzi hizo za chini, wagombea wa Halmashauri Kuu Taifa (NEC) na nyadhifa nyingine za juu kwenye jumuiya za chama wanaonekana kujinadi na kuomba kura kupitia vipeperushi kwenye mitando hasa kwenye makundi ya wanaCCM.

Nafasi ambayo inavuta wagombea wengi ni nafasi 15 za wajumbe wa NEC Tanzania Bara inayogombea na wanaCCM 50 na wengine 15 kutoka Zanzibar. Wengine wanawania uongozi wa Umoja wa Wanawake (UWT) na UV-CCM.

Baadhi ya wagombea ambao Mwananchi imeona vipeperushi vyao ni Stephen Wassira, Dk Fenella Mkangala, Angela Akilimali, Esther Baruti na Grace Kingalame.

Kwa kawaida nafasi hizo za NEC ndizo huwa na kinyang’anyiro kikali na safari kitambanisha sura nyingi mpya baada ya wale wakongwe kutokuwamo ama kutokana na kuwa na nafasi nyingine za uongozi, kutokuomba au kuenguliwa.

Katika mabadiliko kadhaa yaliyofanywa na chama hicho, wanachama wake hawaruhusiwi kuwa na kofia mbili kwa mtu mmoja.

Wakongwe waliokuwa wanashikilia nafasi hiyo na wanawania tena ni Wassira, Jackson Msome na Mkangala. Washindi wataungana na wenzao waliochaguliwa mikoani na kutimiza idadi ya wajumbe 162 wa NEC baada ya kupunguzwa kutoka 388 wa awali. Katibu wa Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole hakupatikana kuzungumzia hali hiyo iwapo ni ruksa kufanya hivyo, lakini Akilimali alilieleza Mwananchi kwamba kwa hatua ya sasa baada ya uteuzi wa majina kufanywa na Halmashauri Kuu ya Taifa wanaruhusiwa kujinadi.

Takukuru watia mguu

Mbali na wajumbe kujinadi, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) nayo imepiga kambi katika uchaguzi ili kukabiliana vitendo rushwa.

Mara kadhaa maofisa wa Takukuru katika mikoa mbalimbali wametoa taarifa za kufuatilia vitendo hivyo na wiki iliyopita mkoani Mwanza walilipekua gari la mwenyekiti wa CCM wa mkoa huo, Anthony Diallo.

Katika mabadiliko yaliyoasisiwa na Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli, chama hicho kilipiga marufuku ya matumizi ya fedha katika uchaguzi.