Msigwa aripoti Polisi tena leo, aachiwa

Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa

Muktasari:

Msigwa ambaye ameunganishwa na watuhumiwa wengine tisa akiwemo Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha) Iringa Mjini, Leonce Marto wanatuhumiwa kuratibu utekelezwaji wa matukio mawili ya kihalifu.

Iringa. Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msigwa leo Januari 23, 2018 ameripoti kituo cha Polisi cha kati mkoani hapa kwa ajili ya kuhojiwa, ikiwa ni kutii agizo la masharti ya dhamana aliyopewa baada ya jana kushikiliwa kwa saa kadhaa na kisha kuachiwa.
Msigwa ambaye ameunganishwa na watuhumiwa wengine tisa akiwemo Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (Bavicha) Iringa Mjini, Leonce Marto wanatuhumiwa kuratibu utekelezwaji wa matukio mawili ya kihalifu.
Tukio la kwanza ni la Januari 17 la kuchomwa kwa nyumba aliyokuwa akiishi Katibu wa Jumuiya ya Vijana wa CCM Iringa Mjini, Alfonce Muyinga.
Akizungumza na Mwananchi Kamanda wa Polisi mkoani Iringa,  Julius Mjengi amedai tukio jingine ambalo Msigwa ameratibu ni lile la Januari 15 la kubomolewa kwa nyumba ya aliyekuwa Diwani wa Kata ya Mwangata Chadema, Anjelus Mbogo aliyejiuzulu nafasi yake na kuhamia CCM.
"Tulimshikilia jana kwa mahojiano na kumuachia saa tatu usiku lakini leo aliripoti kituoni na atakuwa akiripoti wakati taratibu nyingine zikiendelea kama sehemu ya kutii masharti ya dhamana aliyopewa,” amesema.
Alipotafutwa na Mwananchi Msigwa amesema, “Leo siko katika hali nzuri kulizungumzia hilo nafikiri mngesubiri hadi kesho nikiripoti kituoni nitakuwa na wakati mzuri wa kuzungumza.”