Msimamo wa Askofu Munga waibua hisia za raia kuhusu amani

Muktasari:

Katika ibada maalumu ya kuliombea amani Taifa iliyofanyika katika Kanisa la KKKT jijini Tanga juzi jioni, askofu huyo aliweka bayana kwamba Serikali haiwezi kukwepa lawama kutokana na matukio yanayotokea nchini kwa kuwa inao wajibu wa kulinda raia.

Kitendo cha Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Kaskazini Mashariki, Dk Stephen Munga kuzungumzia hali ya usalama nchini na kuweka bayana msimamo wake, kimepongezwa na wananchi na kutaka viongozi wa madhehebu mengine kuiga mfano huo.

Katika ibada maalumu ya kuliombea amani Taifa iliyofanyika katika Kanisa la KKKT jijini Tanga juzi jioni, askofu huyo aliweka bayana kwamba Serikali haiwezi kukwepa lawama kutokana na matukio yanayotokea nchini kwa kuwa inao wajibu wa kulinda raia.

Alisema matukio ya kuchomwa mabweni ya wanafunzi, kupigwa risasi kwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu na Meja Jenerali mstaafu wa JWTZ, Vincent Mritaba na kutekwa kwa watoto mkoani Arusha, yamewatia hofu wananchi.

Alisema Serikali inao wajibu wa kudhibiti matukio kama hayo yasitokee na kuonya kwamba yakiachwa, yanaweza kuifanya Tanzania kuwa kama nyumba iliyoingiwa na joka linalowagonga na kuwaua watoto, huku likiwa halionekani na kuzua hofu kubwa.

Alisisitiza kuwa amani iliyopo ni lulu isiyotakiwa kuachwa ipotee.

Katika maombi hayo ambayo waumini walifurika kanisani hapo na kulazimika wengine kusimama nje, waliwaombea wanaoendesha unyama dhidi ya wasiokuwa na hatia waangamizwe.

Wakizungumza kuhusiana na mahubiri hayo, baadhi ya wakazi wa Tanga walisema Askofu Munga ameonyesha njia kwa viongozi wengine, “Ninachojua hata kwa masheikh kuna hadithi zinazowatahadharisha kuwa kila mchunga, siku ya kiyama ataulizwa aliwachungaje aliokuwa akiwaongoza ili wasipotee, kama hakutekeleza hilo atambue kuwa hakuna atakayemtetea,” alisema muumini wa kanisa hilo, Julius Mjata.

Mkazi mwingine, Ramadhani Manyeko alisema sheikh au askofu asiyepaza sauti kutokana na hali ilivyo hivi sasa, ajitathmini upya kama anatosha.