Mtwara yashika mkia matokeo kidato cha pili

Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde

Muktasari:

Baraza hilo pia limetangaza matokeo ya upimaji wa kitaifa wa darasa la nne ambapo jumla ya wanafunzi 950,167 sawa na asilimia 93.36 wamepata alama za madaraja ya ufaulu zitakazowawezesha kuendelea na darasa la tano.

Dar es Salaam. Katika matokeo ya kidato cha pili 2016 yaliyotangazwa na Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), Mkoa wa Mtwara umeshika mkia kitaifa.

 Baraza hilo pia limetangaza matokeo ya upimaji wa kitaifa wa darasa la nne ambapo jumla ya wanafunzi 950,167 sawa na asilimia 93.36 wamepata alama za madaraja ya ufaulu zitakazowawezesha kuendelea na darasa la tano.

Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde amesema wanafunzi 372,228 kati yao wasichana 189,161 (90.27%) na wavulana 183,067 (91.80%) wamepata ujuzi na maarifa ya kuwawezesha kuendelea na kidato cha tatu.

Kwa mujibu wa matokeo hayo kati ya shule 10 za sekondari zilizofanya vibaya kwenye mtihani huo, tisa zinatoka katika Mkoa wa Mtwara na moja Tanga. Alizitaja shule hizo za Mtwara zilizofanya vibaya kuwa ni Chingungwe, Malocho, Naputa, Chanikanguo, Mtiniko, Michiga, Msimbati, Salama na Lukodoka  huku ya Tanga ikiwa ni Nywelo.