Mugabe ameandaa barua ya kujiuzulu

Muktasari:

Viongozi wawili waandamizi wa serikali ya Mugabe waliliambia shirika la habari la Reuters Jumapili kwamba Mugabe alikuwa amekubali kujiuzulu lakini hawakuwa wanajua

 

Harare, Zimbabwe. Rais Robert Mugabe amekubali kung’atuka na kwamba ameshaandaa barua ya kujiuzulu, shirika la utangazaji la CNN limeambiwa na chanzo kilichokaribu na timu ya majadiliano upande mmoja wakiwemo majenerali waliotwaa madaraka wiki iliyopita.

Chanzo hicho kimedokeza kwamba majenerali wameridhia matakwa mengi ya Mugabe ikiwa ni pamoja na kupewa kinga ya kutoshtakiwa yeye na mkewe Grace, na abaki na mali zake.

CNN limeambiwa kwamba chini ya makubaliano hayo, Mugabe na Grace hawatashtakiwa. Pia, viongozi wawili waandamizi wa serikali ya Mugabe waliliambia shirika la habari la Reuters Jumapili kwamba Mugabe alikuwa amekubali kujiuzulu lakini hawakuwa wanajua yaliyomo katika mkataba wa kuondoka kwake.

Ili ionekane amejiuzulu rasmi, utaratibu ni kwamba barua lazima iandikwe kwenda kwa Spika wa Bunge, chanzo kingine kimeongeza.

Mugabe ambaye anakabiliwa na shinikizo la kujiuzulu kutoka kila kona aliwashangaza watu Jumapili alipokataa kufanya hivyo alipolihutubia taifa kwa njia ya televisheni akiwa ikulu.

Chama chake cha Zanu PF kimempa Mugabe, ambaye amekuwa katika kizuizi cha nyumbani na jeshi lililotwaa madaraka kimempa hadi mchana leo kuondoka vinginevyo atashtakiwa bungeni.

Jumamosi, maelfu ya Wazimbabwe walijimwaga mitaani kupaza sauti zao wakimtaka mzee huyo mwenye umri wa miaka 93, ajiuzulu.