VIDEO-Watatu wafa kwa mvua Dar

Muktasari:

Kamanda Mambosasa amesema wazazi wawachunge watoto na kuwazuia kucheza kwenye vyanzo vya maji.

Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa amesema miili ya watu watatu imeokotwa katika eneo la Tabata Kisiwani jijini Dar es Salaam.

Akizungumza leo Aprili 15 na MCL Digital, Kamanda Mambosasa amesema uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa watu hao wamefariki dunia kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha jijini hapa.

Amesema, miongoni mwa waliofariki ni mama na mtoto ambao wameangukiwa na ukuta wa nyumba yao.

 “Hizi mvua zinazoendelea kunyesha zimeleta athari kubwa kuna watu watatu wote wanaishi Tabata Kisiwani wamefariki kutokana mvua zinazoendelea kunyesha, hivyo ninawaomba watu kuwa na tahadhali wanapoona maji yamejaa wasijaribu kuvuka,” amesema

Mambosasa amesema tukio hilo lilitokea usiku wa kuamkia leo na polisi walipelekewa taarifa na wasamaria wema ndipo walikwenda kwenye tukio na kukuta mama akiwa na mwanaye wameangukiwa na ukuta wa nyumba, eneo la Tabata Kisiwani.

Pia katika tukio jingine mwili wa mwanaume mwenye umri wa kati ya miaka 20 hadi 25 umekutwa ukiwa unaelea kwenye mto Msimbazi .

Kamanda Mambosasa amewaonya wazazi wasiwaruhusu watoto kucheza kwenye maji na madimbwi katika kipindi hiki cha mvua.