Mwakyembe afumua mtandao wa ‘unga’

Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe akizungumza na waandishi wa habari jana kuhusu usafirishaji wa madawa ya kulevya unavyofanyika katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam

Muktasari:

Alisema mizigo ikishaondoka mikononi mwa abiria hukaguliwa tena kwa kutumia mbwa wa Idara ya Usalama wa Taifa, lakini siku ya tukio hilo mbwa hao walichelewa na walitumika baada ya mizigo kuingizwa kwenye masanduku ya chuma.

Dar es Salaam. Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe jana ameanika majina ya watu saba waliohusika kupitisha mabegi tisa yaliyokuwa na kilo 180 za dawa za kulevya zenye thamani ya Sh8 bilioni, Julai 5 mwaka huu katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), wakiwamo maofisa usalama wanne wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) na polisi mmoja.

Alisema mizigo ikishaondoka mikononi mwa abiria hukaguliwa tena kwa kutumia mbwa wa Idara ya Usalama wa Taifa, lakini siku ya tukio hilo mbwa hao walichelewa na walitumika baada ya mizigo kuingizwa kwenye masanduku ya chuma.

“Kwa abiria watatu kuwa na mabegi makubwa tisa yanayofanana si kitu cha kawaida kukwepa jicho la maofisa wa ushuru wa forodha na vyombo vya usalama, sijui walikuwa wapi siku hiyo?” alihoji Mwakyembe.

Juzi waziri huyo aliahidi kuyaweka hadharani majina ya watu wanaosafirisha dawa za kulevya nchini, na alitekeleza ahadi hiyo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari, kusema kuwa watu hao wamenaswa baada ya mfumo wa kamera (CCTV) za uwanja huo kudaka matukio kadhaa yaliyotokea siku ya tukio hilo, kuanzia saa 9:25 hadi saa 10:30 alfajiri.

Ameagiza wafanyakazi hao wanne pamoja na askari polisi mwenye cheo cha koplo, mbeba mizigo na mfanyabiashara aliyekuwa na wasichana wawili waliokamatwa Afrika Kusini, (ambao hatuwezi kuwataja kutokana na kushindwa kuwapata kujieleza) kuchukuliwa hatua za kinidhamu, kukamatwa na kuunganishwa na watuhumiwa waliokwenda na mzigo huo Afrika Kusini.

Mabegi hayo yaliyokuwa na dawa za kulevya aina ya ‘Crystal Methamphetamine’, yalipitishwa na wasichana wawili wasanii aliowataja kuwa ni Agnes Gerald ‘Masogange’ na Melisa Edward ambao walidakwa siku hiyohiyo katika Uwanja wa Ndege wa Oliver Tambo, Afrika Kusini na tayari wameshafikishwa mahakamani.

Juzi Dk Mwakyembe alifanya ziara JNIA kukagua utendaji kazi kwenye uwanja huo ikiwa ni siku tatu baada ya ahadi aliyotoa akiwa Mwanza kwamba katika kipindi cha wiki mbili, atahakikisha anawakamata vigogo wote walio katika mtandao wa usafirishaji na uingizaji wa dawa za kulevya kupitia viwanja vyote vya ndege nchini.

Saa nane baada ya ziara hiyo, Maofisa wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege wanadaiwa kumkamata Edwin Monyo akiwa na kete 86 za dawa aina ya heroini na misokoto 34 ya bangi aliyokuwa akiisafirisha kwenda Italia kupitia Zurich.

Mpango ulivyosukwa

Alisema siku ya tukio saa 9:28 kamera hizo za usalama zilimwonyesha mbeba mizigo wa uwanja huo akiwa anazungukazunguka eneo la kuingilia abiria kama mtu ambaye ana ahadi na kukutana na mtu fulani.

“Kamera pia zilimnasa ofisa mwingine wa TAA kwa mara kadhaa akitoka na kuingia ndani ya jengo la abiria huku akizungumza na simu, kitendo ambacho hakiruhusiwi kabisa kwa wafanyakazi wa eneo la ukaguzi wa abiria,” alisema na kuongeza;

“Wakati huohuo, kamera zilikuwa zinamwonyesha askari polisi anayetuhumiwa kuhusika katika mpango huo akiwa anarandaranda eneo la uhakiki wa hati za kusafiria kama vile anasubiri kitu fulani.”

Alisema ilipofika saa 10:15 walionekana Agnes na Melisa wakiwa na mfanyabiashara huyo katika eneo la kuingilia abiria huku wakiwa na mizigo na mabegi tisa yaliyofanana.

Alisema kuwa kamera zilimwonyesha polisi huyo akihangaika kuwasaidia abiria mbalimbali kuweka mizigo yao kwenye mashine ya ukaguzi, kazi ambayo alieleza kuwa haikuwa yake.

“Mbeba mizigo anayetuhumiwa kuwa katika mtandao huo alionekana akiwasaidia vijana hao watatu (Agnes, Melisa na mfanyabiashara) kupeleka mizigo yao kwenye mashine ya ukaguzi na baadaye kuyazungushia mabegi hayo katarasi za nailoni na kuyafikisha kaunta ya Shirika la Ndege la Afrika Kusini,” alisema.

Alisema kamera hizo zilimnasa ofisa wa TAA akimwondoa katika kiti cha ukaguzi wa mizigo mfanyakazi mwenzake, na kukaa yeye ikiwa ni dakika chache kabla ya mabegi tisa ya vijana hao hayajaingia katika mashine ya ukaguzi.

“Kinyume na taratibu ofisa huyo hakujiandikisha kwenye kitabu cha wakaguzi (Screener’s logbook), saa 10:16 akaanza kupitisha mabegi hayo tisa mpaka saa 10:22. Alipomaliza kupitisha mizigo hiyo kwa dakika sita akamwachia ofisa aliyekuwa katika eneo hilo na kuondoka,” alisema Dk Mwakyembe.

Alisema ofisa huyo baada ya kuondoka katika kiti hicho alizungumza kwa dakika kadhaa na askari polisi anayedaiwa kuwa katika mtandao huo na kurejea tena sehemu aliyokaa ofisa mwenzake wa TAA na kumnong’oneza jambo fulani.

“Baada ya hapo akaelekea ukumbi wa abiria huku akiongea na simu, mambo hayo yote yalifanyika huku kiongozi wa sehemu ya ukaguzi akiwa hapohapo bila kushtuka,” alisisitiza.

Alisema baada ya mizigo hiyo kupita katika mashine ya ukaguzi (baggage screening machine), vijana wale watatu wakahamia na mizigo yao kwenye kaunta ya Shirika la Ndege la Afrika Kusini.

“Mabegi matatu ya kilo 20 kila moja yalipitishwa yakabaki mabegi sita ambayo yalitakiwa yalipiwe malipo ya uzito wa ziada. Kwa taratibu za shirika hilo kila kilo moja inayoongezeka hulipiwa dola 5 (Sh8,000), vijana wale walitakiwa kulipia dola 600, lakini walitozwa dola 94 tu ambazo zinathibitishwa na risiti tuliyonayo,” alisema.

Alisema katika hali isiyokuwa ya kawaida mfanyabiashara ambaye hakuwa na tiketi ya kusafiri siku hiyo, baadaye alibadili mawazo hapohapo na kuamua kuondoka siku hiyo kwenda Afrika Kusini na kulipia gharama ya dola 60 (Sh96,000) ili kupata tiketi.

“Kutokana na hali hiyo mhakiki wa nyaraka za safari nje ya ukumbi wa abiria siku hiyo, hakupaswa kumruhusu mfanyabiashara kuingia ndani ya ukumbi bila tiketi ya siku hiyo,” alisema na kuongeza;

“Kwa hali ya kawaida mizigo ikishaondoka mikononi mwa abiria hukaguliwa tena kwa kutumia mbwa, lakini siku hiyo mbwa walichelewa na walikuja kutumika baadaye ikiwa ni baada ya mizigo kuingizwa kwenye masanduku ya chuma.”

Hatua za wizara

Alisema wizara imeagiza TAA kuwa, kuanzia sasa mtu yeyote anayekamatwa na dawa za kulevya lazima apigwe picha na zisambazwe kwenye vyombo vya habari.

Pia ameliagiza Jeshi la Polisi kushirikiana na Polisi wa Kimataifa (Interpol) kumkamata mfanyabiashara anayedaiwa kuwasaidia Masogange na mwenzake kusafirisha dawa za kulevya ambaye alitoweka na mabegi matatu ya dawa hizo huko Afrika Kusini, “Akamatwe na kuunganishwa na kesi inayowakabili Watanzania hao wawili.”

Alisema mbeba mizigo anatakiwa kufukuzwa kazi na mwajiri wake na asiruhusiwe kukanyaga JNIA, kwamba serikali imewaagiza polisi kumkamata mtu huyo kwa lengo la kuunganishwa na wenzake kujibu mashtaka ya jinai chini ya sheria ya kuzuia dawa za kulevya, sura ya 95 ya mwaka 1996.

Alisema TAA inatakiwa kuwafukuza kazi mara moja wafanyakazi wake wanne waliohusika katika mpango huo, kuwakamata na kuwaunganisha katika mashtaka yanayowakabili.

“Jeshi la polisi limeagizwa kumwondoa mara moja askari mwenye cheo cha koplo anayedaiwa kuhusika katika tukio hilo na kumchukulia hatua za kinidhamu kwa kushiriki kwake kwa njia moja au nyingine kwenye njama za kupitisha mabegi hayo ya dawa za kulevya,” alisema.

Alifafanua kuwa Idara ya Usalama wa Taifa imeagizwa kuendesha uchunguzi wa kina kwa maofisa wake waliokuwa zamu siku ya tukio kwa kuchelewa kuwafikisha mbwa wakati mwafaka, jambo ambalo limeliletea taifa fedheha kubwa.

“Serikali imeziagiza taasisi zote zilizopo chini ya JNIA kutekeleza majukumu ipasavyo na kwa mujibu wa sheria na taratibu ili kuhakikisha dawa za kulevya hazipiti kwenye kiwanja hicho kikuu cha ndege nchini,” alisisitiza.