Mwalimu aliyemtwanga makonde mwenzie apandishwa kizimbani

Muktasari:

Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya ya Serengeti, Ismael Ngaile mshtakiwa amedaiwa kutenda kosa hilo Desemba 6 mwaka huu, alipomvamia mwalimu Marwa ofisini kwake na kumshambulia kwa ngumi hadi kumsababisha jeraha katika jicho lake la kushoto.

Serengeti. Mwalimu Yaredi Amosi (27), wa Shule ya Msingi Kitarungu amepandishwa kizimbani leo Jumanne kwa kosa la kumshambulia kwa ngumi na kumsababishia majeraha mwalimu mkuu wa shue hiyo, Thomas Marwa.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya ya Serengeti, Ismael Ngaile mshtakiwa amedaiwa kutenda kosa hilo Desemba 6 mwaka huu, alipomvamia mwalimu Marwa ofisini kwake na kumshambulia kwa ngumi hadi kumsababisha jeraha katika jicho lake la kushoto.

Akisoma hati ya mashtaka katika kesi hiyo namba 272/2017, Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Renatus Zakeo amesema kitendo hicho ni kinyume cha kifungu cha 16 cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu kama ilivyorekebishwa mwaka 2002.

Mshitakiwa alikana shitaka hilo na kupelekwa mahabusu hadi Desemba 27 shauri hilo litakapotajwa tena baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili wenye barua za utambulisho na mmoja akiwa ni mtumishi wa Serikali.