Mwalimu sekondari adaiwa kuwapa mimba wanafunzi watano

Muktasari:

Wanafunzi hao wamebainika kuwa na ujauzito, baada ya uongozi wa shule hiyo kuona mabadiliko kwenye miili yao na kuamua kuwapima afya.

Mwanza. Mwalimu wa Shule ya Sekondari ya Nyakabungo wilayani Nyamagana mkoani Mwanza, anatuhumiwa kuwapa ujauzito wanafunzi watano wa shule hiyo.

Wanafunzi hao wamebainika kuwa na ujauzito, baada ya uongozi wa shule hiyo kuona mabadiliko kwenye miili yao na kuamua kuwapima afya.

Mkuu wa shule, Boniphace Mjuli amesema baada ya kujiridhisha kuwa wana ujauzito, waliwaandikia barua wazazi wao kuwaita shuleni kwa ajili ya kuwaeleza matokeo ya vipimo na kuchukua hatua stahiki.

Wakizungumzia tukio hilo, baadhi ya wazazi wa watoto waliokutwa na ujauzito wameiomba Serikali ichukue hatua kwa wanaume wote wanaokatisha ndoto za wanafunzi wa kike.

Mzazi Yusuph Yusuph amesema ili kuwajengea mazingira mazuri wanafunzi wa kike, lazima Serikali itekeleze sheria ya kuwakamata wanaume wenye tabia za kutongoza wanafunzi na wahukumiwe kifungo cha maisha jela ili iwe fundisho.