Mwanafunzi wa Old Tanga auawa, achubuliwa ngozi

Kamanda wa polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe

Muktasari:

  • Aliwaaga wenzake saa mbili usiku kuwa anakwenda kujisomea na atarejea baada ya muda mfupi

Tanga. Mwanafunzi wa kidato cha nne Shule ya Sekondari Old Tanga, Shufaa Mbughuni amekutwa amefariki dunia huku uso wake ukiwa umechubuliwa ngozi.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe amethibitisha kutokea kwa tukio hilo akisema kwamba mwili wa mwanafunzi huyo ulikutwa jana katika Mtaa wa Majani Mapana Kata ya Nguvumali saa 9.40 alasiri.

Kamanda Bukombe alisema taarifa kamili kuhusiana na tukio hilo ataitoa baada ya madaktari wa Hospitali ya Mkoa wa Tanga ya Bombo kuufanyia uchunguzi mwili huo.

“Ni kifo chenye utata hatuwezi kusema ameuawa au vinginevyo, tunasubiri taarifa ya madaktari wa Hospitali ya Bombo watakapouchunguza mwili huo; nitawaeleza habari yote,” alisema Bukombe.

Baba wa mwanafunzi huyo ambaye pia ni mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Majani Mapana, Salim Mbughuni alisema bintiye aliwaaga wenzake juzi saa mbili usiku kwamba anakwenda kujisomea lakini hakurudi kama ilivyo kawaida yake.

“Aliwaaga wenzake kwamba anakwenda kujisomea na atarudi baada ya muda mfupi lakini hakuweza kurejea hadi mwili wake ulipoonekana siku ya pili mtaani hapa akiwa amefariki dunia,” alisema Mbughuni.

Mmoja wa wanafunzi katika shule hiyo, Halima Juma alisema: “Mimi usiku ule nilipigiwa simu ya kuulizwa kama nilimwita Shufaa lakini ukweli ni kwamba sikumwita. Leo hii rafiki yangu ameuawa kikatili namna hii inasikitisha sana.”