Mwanamke ajinyonga akiwa mahabusu

Muktasari:

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea  katika Kituo cha Polisi cha Kati usiku wakati wenzake wakiwa wamelala.

Arusha. Mahabusu Victoria Edward (51), mkazi wa Lemara mkoani hapa, aliyekuwa anatuhumiwa kuchoma moto nyumba ya familia yao, amejinyonga hadi kufa ndani ya chumba cha mahabusu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alisema jana kuwa tukio hilo lilitokea  katika Kituo cha Polisi cha Kati usiku wakati wenzake wakiwa wamelala. 

“Polisi wa zamu alisikia kelele kutoka kwenye chumba cha mahabusu wa kike, walijitahidi kuokoa maisha ya mahabusu, lakini ilishindikana,” alisema.

Mkumbo alisema mahabusu huyo alijinyonga kwa kutumia shuka alilokuwa anatumia kujifunika.

Alisema mtuhumiwa huyo alitarajiwa kupandishwa kizimbani  kusomewa mashtaka yaliyokuwa yanamkabili jana.