Mwanamke azaa watoto 38, aweka rekodi Afrika

Mwanamke aliyejifungua watoto 38 Mariam Nabatanzi Babirye akiwa na baadhi ya watoto wake. Picha ya mtandao.

Muktasari:

  • Kwa mujibu wa kamusi ya Wikipedia mwanamke huyo anashika nafasi ya tisa duniani, ya kwanza Afrika

Kampala, Uganda. Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 37 ametoa changamoto kubwa kwa wanawake wengine baada ya kuzaa watoto 38 na kuweka rekodi barani Afrika huku akishika nafasi ya tisa duniani.

Aliyeweka rekodi hiyo barani Afrika ni Mariam Nabatanzi Babirye, mkazi wa Kijiji cha Kabimbiri, wilayani Mukono nje kidogo ya Jiji la Kampala, Uganda.

Akizungumza na gazeti la Daily Monitor la nchini humo, Babirye alisema mtoto wake wa mwisho alijifungua kwa upasuaji Desemba mwaka jana na madaktari walikata mfuko wake wa uzazi.

Babirye amejifungua watoto pacha mara sita, watoto watatu kwa wakati mmoja mara nne, watoto wanne wakati mmoja mara tatu na mtoto mmoja mara moja. Kati ya watoto hao, 10 ni wasichana na 28 ni wavulana. Mkubwa ana umri wa miaka 23 huku mdogo akiwa na miezi sita.

Mwanamke huyo anasema aliolewa mwaka 1993 akiwa na miaka 12 huku mumewe akiwa na umri wa miaka 40.

“Sikujua kama nilikuwa nimeolewa. Watu walikuja nyumbani na kumletea vitu baba yangu. Wakati wanaondoka nilidhani namsindikiza shangazi, lakini tulipofika huko alinikabidhi kwa mwanamume,” alisema Babirye.

Mwaka 1994, wakati Babirye akiwa na umri wa miaka 13, alijifungua watoto pacha, miaka miwili baadaye alijifungua watoto watatu na mwaka mmoja na miezi saba baadaye alijifungua watoto wanne kwa wakati mmoja.

Hata hivyo, anasema hakuna kilichomshangaza katika uzazi huo kwa kuwa alikuwa ameshawaona wanawake wengine waliozaa watoto wengi katika familia yao.

“Baba yangu alizaa watoto 45 kwa wanawake tofauti na wote walikuwa wakizaliwa watano, wanne, watatu na wawili kwa mara moja,” alisema Babirye ambaye anafahamika zaidi kwa jina la Nalongo Muzaala Bana likimaanisha ‘mama wa pacha anayezaa watoto wanne wanne’.

Mtaalamu wa masuala ya uzazi katika Hospitali ya Mulago nchini Uganda, Dk Charles Kiggundu alisema upo uwezekano wa mwanamke huyo kurithi uwezo wake wa kuzaa kutoka kwa baba yake. “Suala lake ni la kurithi ambalo linaongeza uwezekano wa kuzaa watoto wengi,” alisema.

Daktari alimwambia mwanamke huyo kuwa hawakuweza kumzuia kuendelea kuzaa kwa kuwa ana kiwango cha juu cha mayai ya uzazi, ambacho kingeweza kumuua kama angeacha kuzaa.

Kwa mujibu wa Wikipedia, anayeshika rekodi hiyo ni Feodor Vassilyev (27), Mrusi aliyezaa watoto 69 akifuatiwa na Rosa Gravata wa Italia aliyezaa watoto 62  na nafasi ya tatu inashikiliwa na  Yakov Kirillov aliyejifungua watoto 57.

Kwa mujibu wa Guinness World Records, Nadya Suleman wa California ndiye ameweka rekodi ya kujifungua watoto wanane kwa wakati mmoja Januari 26, 2009.