Mwenyekiti wa wazee Chadema ahamia CCM akidai imebadilika

Muktasari:

  • Akikabidhi kadi ya Chadema, skafu mbili na fulana mbili za chama hicho kwenye mkutano wa halmashauri ya CCM wilayani hapa, Matius ambaye pia ni mjumbe wa Serikali ya mtaa wa Buhemba alisema ameamua kujiunga na chama hicho kutokana na mabadiliko yanayofanywa na Serikali.

 Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Chadema katika kata ya Bomani wilayani Tarime, Morice Matius amehamia CCM akidai kuvutiwa na mabadiliko ya chama hicho.

Akikabidhi kadi ya Chadema, skafu mbili na fulana mbili za chama hicho kwenye mkutano wa halmashauri ya CCM wilayani hapa, Matius ambaye pia ni mjumbe wa Serikali ya mtaa wa Buhemba alisema ameamua kujiunga na chama hicho kutokana na mabadiliko yanayofanywa na Serikali.

Alisema moja ya ajenda iliyokuwa ikizungumzwa na Chadema kipindi cha nyuma ni kutokuwapo kwa ndege za Serikali, mikataba mibovu ya madini na kero zingine ambazo zimeanza kutatuliwa huku nyingi zikiwa zinapatiwa ufumbuzi.

Mkuu wa wilaya ya Tarime, Glorius Luoga alisema kila mwanachama wa CCM anatakiwa kwenda na kasi ya Serikali iliyopo madarakani.

Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) Wilaya ya Tarime, Godfrey Frances alisema moja ya sababu ya upinzani kushinda kwenye chaguzi ni kutokana na baadhi ya viongozi wa CCM kutokuwa tayari katika kutetea masilahi ya wananchi.