Mwenyekiti wazee Chadema ainanga CCM

Muktasari:

Adai mipango inasukwa kuiunganisha Chadema na CUF Zanzibar kuwa kitu kimoja kuibwaga CCM

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Baraza la Wazee la Chadema, Hashim Juma  amesema Chama Cha Mapinduzi (CCM) hakijiamini ndiyo maana kinapoteza mabilioni ya fedha kurejea kwenye uchaguzi wakati Watanzania wana shida nyingi.

Akihutubia katika mkutano wa kampeni za ubunge wa Ukonga leo kumnadi Asia Msangi anayegombea kupitia chama hicho alisema: “Hakukuwa na sababu za kurudia huu uchaguzi mambo haya yalishaishia 2015.

Aidha, Mwenyekiti huyo wa wazee Chadema alivitaka vyombo vya dola kujiweka kando na uchaguzi huo.

 “Tunawaambia kwamba hapa Ukonga hatutaruhusu vyombo vya dola vituingilie tutakula nao sahani moja,” alisema.

Juma alirejea kile alichosema juzi  kumkaribisha Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad kujiunga na Chadema.

“Tunafanya mpango wa kuiunganisha Chadema na CUF kule Zanzibar iwe kitu kimoja ili tuiangushe CCM.”

Naye mratibu wa Chadema, Kanda ya Pwani, Casmir Mabina alidai CCM imekuwa ikinunua madiwani na wabunge wa vyama vya upinzani halafu baadaye wanawarudishwa kwa mlango wa nyuma wagombee tena nafasi walizoacha kupitia chama hicho tawala.

 “Hawa ni waoga kweli kweli, sasa tunasema kama unataka kuondoka tuambie tukufanyie ‘Send off’ ili uondoke kwa amani siyo kwa kujifichaficha,” alisema.

Aliwataka wananchi wa jimbo hilo kutompa kura mgombea wa CCM, Mwita Waitara ambaye alikimbia Chadema na kuachia ubunge ambao anagombea tena kupitia chama chake hicho kipya.

 “Mpuuzeni Waitara, tumesikia analalamika kwamba mabango yake yanaharibiwa, sasa kama amewatumikia wana Ukonga kwa miaka miwili kuna haja kweli ya kulilia mabango?” alihoji Mabina