Mwili wa Mpigapicha Mkuu wa Tanzania Daima kuagwa leo

Muktasari:

Kwa mujibu wa Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Neville Meena mwili huo unatarajiwa kuagwa kuanzia saa  Tatu asubuhi katika uwanja wa mpira uliojirani na nyumbani kwa marehemu Senga, Sinza.

Dar es Salaam. Mwili wa aliyekuwa Mpigapicha Mkuu wa Gazeti la Tanzania Daima, Joseph Senga (58) unaagwa leo jijini Dar es Salaam.

Kwa mujibu wa Mhariri Mtendaji wa Gazeti la Tanzania Daima, Neville Meena mwili huo unatarajiwa kuagwa kuanzia saa  Tatu asubuhi katika uwanja wa mpira uliojirani na nyumbani kwa marehemu Senga, Sinza.

“Saa tano utasafirishwa kuelekea nyumbani kwao Shushi-Nyambichi, Kwimba mkoani Mwanza kwa ajili ya maziko yatakayofanyika kesho,” alisema Meena.

Awali, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye aliwaongoza mamia ya wakazi wa Jiji la Dar es Salaam kupokea Mwili huo uliowasili jana katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), ukitokea New Delhi, India kwa ndege ya Shirika la Ethiopia Airlines. Senga, alifariki dunia Julai 27 nchini humo alikokwenda kupatiwa  matibabu ya moyo Julai 19.