Mzazi adai kuzuiwa kutoka wodini baada ya kujifungua watoto watatu

File Photo

Muktasari:

Madai hayo yamekuja licha ya Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu kutoa agizo la kutowatoza fedha wajawazito.

Dar es Salaam. Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imedaiwa kumzuia kutoka wodini Lucy Samson (25) aliyejifungua kwa upasuaji watoto watatu tangu Agosti 24 mwaka huu, ikimdai Sh375,540.

Madai hayo yamekuja licha ya Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu kutoa agizo la kutowatoza fedha wajawazito.

Akitoa agizo hilo Agosti 22 wakati akielezea kuhusu mapitio ya Sera ya Afya ya mwaka 2007, Mwalimu alipiga marufuku kuwatoza fedha wajawazito, watoto chini ya umri wa miaka mitano na wazee wasiojiweza huku akisema atamchukulia hatua mganga mkuu yeyote wa mkoa au mfawidhi atakayekiuka agizo hilo.

 Lucy amesema alilazwa tangu Julai 24 kabla ya kujifungua lakini amezuiwa kwa kushindwa kulipa deni hilo.

Alipotafutwa Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili ili kutoa ufafanuzi kuhusu mgonjwa huyo, hakupatikana na simu yake iliita bila kupokewa na baadaye ilikuwa inaita na kukata.