Mzazi asimulia maiti ya mtoto ilivyoachwa chumbani

Vijana wakiwa wamebeba jeneza tupu baada ya kulifukua kutokana na kuzikwa likiwa bila mwili wa marehemu Haruna Kyando (9) aliyekuwa mkazi wa Isanga jijini Mbeya. Picha na Godfrey Kahango

Muktasari:

Mtoto huyo, Haruna Kyando (9), aliyekuwa akisumbuliwa na kifafa kwa muda mrefu, alikutwa chumbani asubuhi ya Jumatatu akiwa amefariki dunia nyumbani kwao Isanga mjini hapa, baadaye waombolezaji waliamua kumzika bila  kutoa heshima za mwisho.

Mbeya.  Mzazi Jailo Kyando (36), ambaye maiti ya mtoto wake iliachwa chumbani na waombolezaji ambao walizika jeneza tupu, amesema huenda wabebaji walitegeana hivyo kutong’amua kuwa halikuwa na mwili wa marehemu.

Mtoto huyo, Haruna Kyando (9), aliyekuwa akisumbuliwa na kifafa kwa muda mrefu, alikutwa chumbani asubuhi ya Jumatatu akiwa amefariki dunia nyumbani kwao Isanga mjini hapa, baadaye waombolezaji waliamua kumzika bila  kutoa heshima za mwisho.

Lakini, baada ya jeneza kupelekwa nyumbani kwa ajili ya kuweka maiti ya mtoto huyo, waombolezaji hawakushughulika na mwili badala yake, walibeba jeneza na kuungana na wengine kwenda kulizika, lakini waliporudi nyumbani, walikuta maiti juu ya godoro hilo kama ilivyokuwa imewekwa kabla ya kwenda makaburini.

Akisimulia tukio hilo, mzazi huyo alisema kifo cha ghafla cha mwanaye kiliwachanganya yeye na mkewe, Anna Elieza (32)  hadi kufikia kushindwa kufanya jambo lolote.