Mzee Majuto azidiwa, alazwa ICU Muhimbili

Muktasari:

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa MNH Aminiel Aligaesha amesema Majuto aliletwa hospitalini hapo Jumanne wiki hii saa 12 jioni.

Dar es Salaam. Msanii maarufu wa maigizo Amri Athuman maarufu ‘King Majuto’ amelazwa chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU) katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Mkurugenzi wa Mawasiliano wa MNH Aminiel Aligaesha amesema Majuto aliletwa hospitalini hapo Jumanne wiki hii saa 12 jioni.

“Ni kweli yupo chumba cha wagonjwa mahututi, tunaye hapa,” amesema.

Ofisa Habari wa Chama cha Waigizaji Kinondoni Masoud Kaftany naye amethibitisha taarifa hizo.

“Tayari madaktari wameanza kufanya vipimo ili kubaini ugonjwa unaomsumbua,” amesema.

Hii ni mara ya pili kwa Mzee Majuto kulazwa MNH, mara ya kwanza alilazwa kabla ya kwenda India kwa upasuaji wa tezi dume.