NEC yasema haiwezi kuahirisha uchaguzi mdogo

Muktasari:

Uchaguzi mdogo wa ubunge katika majimbo matatu na kata sita umepangwa kufanyika Januari 13,2018.

Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Uchaguzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Kailima Ramadhani amesema chama cha siasa kutangaza kugomea uchaguzi hakuwezi kuifanya Tume iuahirishe kwa kuwa haiko kumshawishi mtu au chama kushiriki.

Akizungumza leo Jumanne Desemba 12,2017 jijini Dar es Salaam, Kailima amesema chama kushiriki uchaguzi ni jambo la hiari na NEC ipo kwa ajili ya kuweka na kutengeza mazingira yatakayofanya vyama vya siasa kushiriki uchaguzi.

Kailima katika taarifa iliyotolewa na NEC amesema iwapo kuna chama kitaamua kutoshiriki uchaguzi, kitakachoshiriki hata kama ni kimoja mgombea wake atapita bila kupingwa.

“Ikitokea vyama vikasusa vyote kushiriki kwenye uchaguzi hapo ndipo unaweza kuahirishwa kwa kuwa hakutakuwa na mgombea,” amesema alipozungumza na waandishi wa habari waliotaka ufafanuzi wa NEC kuhusu tamko lililotolewa na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Kailima ameviasa vyama vya siasa vinavyotishia kutoshiriki uchaguzi mdogo wa ubunge katika majimbo matatu na kata sita Januari 13,2018 kufuata mifumo ya kisheria ya kushughulikia malalamiko ya uchaguzi.

Juzi Mbowe alitishia kuwa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) havitashiriki uchaguzi iwapo changamoto zilizojitokeza wakati wa uchaguzi mdogo wa madiwani katika kata 43 Novemba 26,2017 hazitafanyiwa kazi na NEC.

Akizungumzia hoja hiyo, Kailima amesema katika orodha ya vyama vilivyopo NEC, Ukawa si moja ya vyama vya siasa.

“Niwasihi vyama vya siasa watumie mifumo iliyopo ya kawaida ya kuwasilisha malalamiko kwenye kamati za maadili; kujaza fomu namba 14 kabla ya kura kuanza kupigwa; fomu 16 wakati kura zinapigwa; na kuwasilisha malalamiko mahakamani baada ya kura kuhesabiwa,” amesema Kailima.

Amesema hiyo ndiyo mifumo iliyowekwa kisheria katika kushughulikia changamoto za uchaguzi zinapojitokeza na kuhoji wanayotaka wao ni ipi.

“Kama kuna mgombea hakuridhika mahakama zipo aende maana wamepewa siku 30 za kufungua kesi,” amesema.

Amesema NEC haiwezi kuahirisha uchaguzi kwa kuwa sheria inatamka kuwa uchaguzi unaweza kuahirishwa iwapo tu kuna mgombea amefariki; kutokuwepo mgombea; zikitokea ghasia na fujo au wagombea wakifungana kwa kura.

“Je kuna mgombea amefariki? Haya mambo yote manne hayajatokea, sasa tutaahirishaje uchaguzi?” amehoji Kailima.

Kuhusu jimbo la Longido ambalo Mbowe alidai shauri la uchaguzi bado liko mahakamani na wameiandikia NEC kuhusu suala hilo na barua kutojibiwa, Kailima amesema madai hayo si ya kweli kwa kuwa barua zote walizoandikiwa wamezijibu.

Amesema jimbo hilo liko wazi kwa kuwa Mahakama ndiyo imeiandikia NEC kuitaarifu kumalizika kwa kesi iliyokuwepo mahakamani.

Kailima amesema NEC itasimamisha uchaguzi wa jimbo hilo iwapo tu Mahakama itawaeleza wasimamishe mchakato huo.

“Nimesikitishwa na kauli kwamba eti wametuandikia barua sisi Tume ya kusimamisha uchaguzi wa Longido eti hatujawajibu. Tulipata barua kutoka kwa ole Nangole (Onesmo) tukamjibu, tukapata barua kwa wakili wa Ole Nangole nikamjibu; tukapata barua kutoka kwa katibu wa Chadema tukamjibu na nikaongea naye kwenye simu, sasa leo wanaposema hatujawajibu kwa kweli kauli hiyo imenisikitisha,” amesema.