NHC kujenga satelite city mkoani Dodoma

Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemiah Mchechu

Muktasari:

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemiah Mchechu alisema uamuzi wa kuhamia Dodoma umekuja wakati mwafaka kwa kuwa tayari walishaanzisha miradi ya ujenzi mkoani humo.

Dar es Salaam. Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) linakusudia kuanzisha miradi mikubwa ya ujenzi Dodoma ikiwa ni kuunga mkono agizo la Rais John Magufuli la kuhamishia makao makuu ya nchi mkoani humo.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Nehemiah Mchechu alisema uamuzi wa kuhamia Dodoma umekuja wakati mwafaka kwa kuwa tayari walishaanzisha miradi ya ujenzi mkoani humo.

“Sisi ni wajenzi na tunalenga sekta za umma na binafsi, tunakwenda Dodoma kujenga, kwa sasa tumeshajenga nyumba 153 tayari tumeuza baadhi zimebaki 97. Tumejenga pia nyumba 44 wilayani Kongwa na tumenunua eneo la ekari 236 pembeni ya Chuo Kikuu cha Dodoma ambako tutajenga miradi ya satelite kama ya Kawe na Arusha,” alisema Mchechu.