Nabaki Afrika: Mauzo vifaa vya ujenzi yameshuka, ukandarasi yameongezeka

Muktasari:

  • Hayo yamebainishwa na meneja mkuu wa Kampuni ya Nabaki Afrika, Mark McCluskey mwishoni mwa wiki alipozungumza na gazeti hili kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Utalii (Site) ya siku tatu yaliyomalizika mwishoni mwa juma.

 Kutokana na uchumi wa wananchi kubana, biashara ya vifaa vya ujenzi wa nyumba imepungua huku vile vya ukandarasi wa miradi mikubwa ukiongezeka zaidi ya mara dufu.

Hayo yamebainishwa na meneja mkuu wa Kampuni ya Nabaki Afrika, Mark McCluskey mwishoni mwa wiki alipozungumza na gazeti hili kwenye Maonyesho ya Kimataifa ya Utalii (Site) ya siku tatu yaliyomalizika mwishoni mwa juma.

Tangu mwaka huu uanze, McCluskey alisema uuzaji wa vifaa vya ujenzi umepungua kwa asilimia 10 ikilinganishwa na ilivyokuwa mwaka jana.

“Tumeuza asilimia 50 tu ya vifaa hivyo mwaka huu. Hata hivyo vifaa kwa ajili ya ujenzi wa barabara mauzo yake yameongezeka kwa asilimia 1,000 (mara 10 zaidi),” alisema McCluskey.

McCluskey alisema ongezeko katika mauzo ya vifaa vya utengenezaji wa barabara ni matokeo ya mipango na usimamizi wa Rais John Magufuli ambaye anatekeleza miradi mingi ya aina hiyo sanjari na kusimamia ubora.

Kuhusu kusambaza na kupigia debe bidhaa zinazotengenezwa nchini McCluskey alisema kipaumbele chao kwenye bidhaa yoyote bila kujali ilikotengenezwa ni ubora.

“Kuna bidhaa kadhaa tunachukua nchini lakini nyingine tunaagiza kutoka nje ya nchi kupata ubora stahiki ambao unatufanya tuendeee kuwa imara sokoni. Katika utengenezaji wa baadhi ya bidhaa inahitajika teknolojia ya hali ya juu ambayo wakati mwingine inakuwa bado haijafika nchini,” alisema McMluskey.