Nafasi za makamishna wa IEBC kujazwa
Muktasari:
Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 19 mwenyekiti wa kamati hiyo William Cheptumo amesema hatua hiyo ni sehemu ya mikakati ya kusuluhisha changamoto zinazoikumba tume hiyo kwa sasa.
Nairobi, Kenya. Kamati ya Bunge kuhusu Haki na Masuala ya Sheria (JLAC) imeanzisha mchakato wa marekebisho ya sheria ya Tume huru na Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwa lengo la kujaza nafasi ya makamishna watatu waliojiuzulu.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Aprili 19 mwenyekiti wa kamati hiyo William Cheptumo amesema hatua hiyo ni sehemu ya mikakati ya kusuluhisha changamoto zinazoikumba tume hiyo kwa sasa.
‘’Kamati hii ambayo ndiyo hufuatilia utendaji kazi wa IEBC inafahamu kuwa tume hiyo sasa imelemazwa kufuatia kujiuzulu kwa makamishna hao,sasa hao watatu waliobakia hawawezi kufanya uamuzi unaoweza kutambulika kisheria na ndiyo maana tumeanzisha mchakato wa kuifanyia kazi marekebisho sheria ya IEBC ili kujaza nafasi za waluiojiondoa’’alisema Cheptumo ambaye ni mbunge wa Baringo Kaskazini’’amesema .
Amesema hayo baada ya mwenyekiti wa Tume hiyo Wafula Chebukati kutofika mbele ya kamati hiyo kuwafafanulia wanachama wake kuhusu mzozo uliosababisha kujiuzulu kwa makamishna Consolata Maina,Dk Paul Kurgat na Margaret Mwachanya.
Vilevile Chebukati na wenzake wamedaiwa kwamba walipaswa kufuatilia kilichosababisha Ofisa Mkuu Mtendaji wa Tume hiyo Ezra Chiloba kupewa likizo.
Kupitia barua ambayo nakala yake iliyotolewa kwa waandishi wa habari Chebukati na wenzake waliomba radhi kwamba wasingeweza kufika mbele ya tume hiyo kwa sababu walikuwa wakisimamia chaguzi ndogo huko Ruguru na Kindono.
Hata hivyo, Cheptumo na wanachama wa kamati yake walikubaliana na ombi hilo na kuahidi kupanga tarehe nyingine ya kumtaka afike mbele ya kamati hiyo.