Nape asema hata hamia upinzani

Muktasari:

Nape amewaambia upinzani kuwa wajipange hana mpango wa kuhama CCM

Mtwara. Mbunge wa Mtama (CCM), Nape Nauye amesema hana mpango wa kuhama CCM kwenda upinzani na badala yake ametaka vyama hivyo visipoteze muda kudhania atahama.

Nape ametoa kauli hiyo jana Jumatatu jioni wakani wa kampeni za kumnadi mgombea udiwani wa Kata ya Reli, Genfrid Mbunda katika uwanja wa Manispaa ya Mtwara Mikindani.

Alisema wapinzani wasipoteze muda wakimsubiri kuwa atahama CCM kutokana kwamba CCM ni chama bora kuliko vyama vyote vya siasa hivyo hawezi kutoka ndani ya chama hicho.

“Unajuwa wapinzani wasipoteze muda wa kusubiri mimi lini nitahama CCM badala yake wafanye kazi ya kuvijenga vyama vyao kwa sababu walitamani sana muziki huu uhamie kwao ndio maana wanabaki wanapiga kelele za kuwapa presha wanaCCM hivyo sitahama kwa sababu ukinikata mwili wangu damu yangu unakuta CCM,” alisema Nape.

Alisema kuwa CCM hakwenda kwa bahati mbaya kutokana kwamba anakijua chama hicho hivyo hakuna namna yoyote itakayoweza kumtenganisha na chama hicho.

“Kupitia changamoto katika mabonde na mawimbi ndio unaandaliwa kuwa mkomavu na kupanda juu kwa sababu ukikimbia mapema unaonekana haufahi lakini ukibaki na kuvulimia milima na mabonde ndio unaokana ni mkomavu na ukizingatia ndani ya chama hiki kuna fursa za kutosha,” alisema.  

“Kupitia mabonde na milima bila kuyumba nitaendelea kusimama imara ndio maana nikaaminiwa sasa wanaodhani Nape anapitia milima na mabonde kwa sababu hata mbegu ili iote ni lazima upande chini ili iweze kuota na hiyo ndio fomula ya maisha sasa wakati mbegu inaoza watu wanaanza kuongea siji ng’o,” aliongeza Nape.

“Mimi bado sijaona mawimbi yanayoweza kumkimbiza  CCM bado nimesimama imara kwa ajili ya kupambana na mawimbi hakuna mabadiliko yasiyo na machungu hata mama mjazito hupata machungu lakini hufurahi kupata mtoto baada ya kuvumilia kwa muda mrefu,” alisema Nape.