Nchemba ashangazwa na kituo cha polisi

Muktasari:

  • Wilaya ya mkalama ina jumla ya askari Polisi 84.
  • Waziri Mwigulu amejionea hali ambayo si nzuri ya kituo cha polisi cha wilaya ya mkalama ambayo ni wilaya mpya iliyomegwa kutoka wilaya ya Iramba.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mwigulu Nchemba ametembelea kituo cha polisi cha wilaya ya mkalama mkoani singida kuangalia hali ya kituo na utendaji kazi wa askari polisi na mazingira wanayofanyia kazi askari hao.

Waziri Mwigulu amejionea hali ambayo si nzuri ya kituo cha polisi cha wilaya ya mkalama ambayo ni wilaya mpya iliyomegwa kutoka wilaya ya Iramba.

Waziri huyo alisema kwamba kituo hiki cha wilaya ya mkalama hali si nzuri kwani ni chakavu sana na kidogo ambacho kina mahabusu moja ya wanaume tu huku wanawake wakiwekwa mapokezi.

Waziri Mwigulu amesema atakaa na wenzake wa wizarani akiwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Simon Sirro kupanga utaratibu wa kumalizia ujenzi wa vituo vyote polisi ambavyo ujenzi wake umekwama hasa wa hizi wilaya ya mpya ambazo zimemegwa katika wilaya mama.

 Amewahidi kamati ya ulinzi na usalama ikiongozwa na mkuu wa wilaya ya mkalama kuwa ujenzi wa kituo hicho utaisha na anakwenda kuonana na IGP kupanga kumalizia ujenzi wa vituo hivyo mapema.

Naye Kamanda wa Polisi wilaya ya Mkalama (OCD) John Ntilima amesema kwasasa wanatumia kituo kidogo cha polisi Nduguti kama kituo cha polisi cha wilaya ambacho ni kidogo sana hakitoshelezi kwa ufanyaji kazi wake kwani wanatumia ofisi tatu ambazo ni mbovu na chakavu  hivyo wana ujenzi wa kituo kikubwa cha kisasa lakini wamekwama kumalizia na kumuomba waziri awasaidia katika kukamilisha hilo.