Ndalichako apigilia msumari makato ya wanufaika bodi ya mikopo

Muktasari:

  • Ndalichako ameliambia bunge kuwa serikali haina mpango wa kupunguza makato hayo ya asilimia 15 kwa wanufaika wa bodi ya mikopo.

Dodoma. Mbunge wa Mbozi Paschal Haonga (Chadema) ameitaka serikali kusitisha makato ya asilimia 15 ya wanufaika wa Bodi ya Mikopo kwani inawaumiza wafanyakazi.

Hata hivyo Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Joyce Ndalichako ameliambia bunge leo Septemba 12, 2018 kuwa serikali haina mpango wowote wa kupunguza makato hayo.

Katika swali la msingi Haonga amehoji iwapo serikali haioni kwamba imevunja mkataba kinyume na makubaliano kwa kuwa wakopaji walisaini mkataba wa asilimia 8 na siyo 15.

 Amesema makato hayo yamekuwa yakiwaathiri kwa kiasi kikubwa wafanyakazi na kusababisha ufanisi wa wafanyakazi kuwa ni mdogo hivyo akataka mpango huo usitishwe mara moja.

Waziri Ndalichako amesema makato ya asilimia 15 kutoka kwenye mshahara ghafi wa mfanyakazi ni ya kisheria yenye lengo la kuhakikisha fedha zinazotolewa na serikali zinarejeshwa kwa wakati ili  ziwasomeshe watanzania wengine.