Vyuo vyapewa siku saba kurejesha Sh 3.8 bilioni za wanafunzi ‘hewa’

Dar es Salaam. Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetoa siku saba kwa vyuo 31 kurejesha Sh3.8 bilioni ambazo vyuo hivyo vilipokea kwa mwaka wa masomo 2015/16, kwa ajili ya wanafunzi 2, 192 ambao hawapo katika vyuo hivyo.

Agizo hilo limetolewa na Waziri wa wizara hiyo, Profesa Joyce Ndalichako ambaye amesema hatua hiyo imekuja baada ya wizara yake kwa kushirikiana na maofisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini  (Takukuru) na Bodi ya Mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu, kufanya uhakiki wa wanafunzi hao.

Profesa Ndalichako amesema katika uhakiki huo uliofanywa kwa Mei hadi Julai mwaka huu, wanafunzi hao hawakujitokeza kuhakikiwa hivyo hakuna uhalali wala uthibitisho wa wanafunzi hao 2,192 kuwapo vyuoni.