Necta yatangaza matokeo darasa la saba, ufaulu waongezeka

Muktasari:

Baraza la Mitihani Tanzania (Necta) limetangaza matokeo ya kuhitimu elimu ya msingi ambapo ufaulu umepanda kwa asilimia 4.96 kwa mwaka 2018. Ufaulu wa masomo ya Kiingereza, Hisabati, Sayansi, Maarifa ya jamii wapanda wakati Kiswahili watajwa kushuka

Dar es Salaam. Baraza la Mitihani Tanzania (Necta) limetangaza matokeo ya kuhitimu elimu ya msingi na kubainisha kuwa ufaulu umeongezeka kwa asilimia 4.96.

Ufaulu mwaka 2017  ulikuwa asilimia 72.76 na 2018 ni asilimia 77.72.

Akizungumza leo Jumanne Oktoba 23, 2018 Katibu Mtendaji wa Necta,  Dk Charles Msonde amesema watahiniwa 733,103 waliofanya mtihani huo wamefaulu.

“Watahiniwa 733,103 kati ya 943,318 waliotunukiwa matokeo wamefaulu. Watahiniwa hawa wamepata alama 100 au zaidi kati ya alama 250," amesema.

Amesema kati ya hao wasichana ni 383,830 (asilimia 77.12) na wavulana ni 350,273 (asilimia 78.38).

"Takwimu zinaonyesha kuwa ufaulu katika masomo ya Kiingereza, Maarifa ya jamii, Hisabati na Sayansi umepanda kwa asilimia kati ya 4.03 na 11.92 ikilinganishwa na mwaka jana," amesema.

Ameongeza kuwa ufaulu katika somo la Kiswahili umeshuka kwa asilimia 1.44.

Pia, Necta imewafutia matokeo watahiniwa 357 baada ya kubainika kufanya udanganyifu kwenye mitihani yao na 120 hawakufanya kabisa na watarudia mwakani.